SUAMEDIA

Wataalamu wa Kilimo wametakiwa kutumia taaluma yao kuhamasisha wakulima kutumia Mbegu bora


NA; AYOUB MWIGUNE

Wataalamu wa Kilimo nchini wametakiwa kutumia taaluma waliyonayo kuhamasisha wakulima kutumia Mbegu zilizo thibitishwa na Mamlaka ya Kuthibiti Ubora wa Mbegu (TOSCI) ili kuondokana na changamoto ya wakulima walio wengi kutumia Mbegu zisizo na ubora na kupelekea kupata Mazao machache yasiyo na tija na wengi wao kushindwa kuendelea na shughuli za Kilimo.

Wito huo umetolewa na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa TAMISEMI Prof. Riziki Shemdoe jijini Dodoma katika mkutano wa mwaka wa Umoja wa Wanasayansi wa Mazao na Vipando Tanzania (CROSAT) ambapo ameitaka Jumuiya hiyo kujadili namna bora ya kuimarisha upatikanaji wa mbegu na kuwafikia wananchi kwa urahisi.

Prof. Shemdoe amesema makusanyo mengi ya Mapato yanayotegemewa na Serikali za mitaa yanategemea Kilimo hivyo kutakapokuwa na Mazao na Mbegu bora Serikali za mitaa zitaweza kupata mapato kwa wingi lakini pia kutakuwa na maendeleo katika kaya.

Vile vile Prof. Shemdoe amesema Tanzania inategemea Chakula ambacho kinatokana na Kilimo hivyo Mkutano wa mwaka wa Umoja huo wa Wanasayansi wa Mazao na Vipando Tanzania unabeba majibu ya maswali mengi ambayo Wakulima wanatamani kuyapata kutoka kwa Wataalam hao.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mkuu wa TOSCI Patrick Ngwediah   amewashauri CROSAT kutoa elimu kwa Wakulima juu ya matumizi sahihi ya Mbegu.

Naye Mwenyekiti wa sasa wa CROSAT Prof. Kallunde Sibuga ambaye pia ni  Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo amesema umoja huo ulianzishwa kwa lengo la kuwakusanya pamoja Wanasayansi wa Mimea.

Aidha akielezea kuhusu dhumuni la kukutana Prof. Sibuga amesema lengo hasa ni kupanga Mikakati kuhusu kuboresha Katiba yao ili kuongeza tija katika kilimo cha mazao, kubadilishana mawazo na kuishauri Serikali kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu Mazao.


Katika Video


Post a Comment

0 Comments