SUAMEDIA

SUA yaja na Mradi wa majaribio ya teknolojia ya Tanuri la kukausha mbao kwa nguvu za jua

 

Na: Farida Mkongwe

Katika kuhakikisha mazingira yanaendelea kutunzwa, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Ndaki ya Misitu, Wanyamapori na Utalii imekuja na mradi wa majaribio ya teknolojia ya Tanuri la kukausha mbao kwa nguvu za jua ambayo ni rafiki kwa mazingira kwa sababu inazuia matumizi ya nishati nyingine ambazo zinaharibu mazingira.

                                  

Mradi huo wa majaribio ambao ni wa kwanza hapa nchini umewekwa bayana Agosti 3, 2024 na Mkufunzi Msaidizi kutoka Idara ya Uhandisi Misitu na Sayansi za Mazao ya Misitu, Ndaki ya Misitu, Wanyamapori na Utalii Mbonea Mweta wakati akizungumza na SUA Media katika Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki yanayofanyika  mjini Morogoro.

                                        

Akizungumzia faida za mradi huo Mkufunzi huyo amesema utasaidia kuongeza thamani ya mbao, kupunguza gharama kwa sababu tanuri hilo linatumia nguvu za jua ukilinganisha na matanuri mengine yanayotumia nishati ya umeme au mafuta ya dizeli ambayo siyo rafiki kwa mazingira, pia mbao zitaweza kudumu kwa muda mrefu na hivyo kuzuia ukataji miti wa mara kwa mara.

“Lakini tanuri hili kama nilivyosema linasaidia kupata mbao iliyokaushwa vizuri ambayo ina vigezo vya viwango vinavyotakiwa katika mbao na ukitumia mbao iliyokaushwa ni dhahiri kuwa utapata samani nzuri lakini ukiunganisha mbao ambazo hazijakaushwa vizuri ni wazi kuwa utapata changamoto ya muungo huo kuachia au mbao hizo kuharibiwa na wadudu waharibifu na hivyo kupata hasara”, amesema Mkufunzi huyo.

                                        

Amezitaja fursa nyingine zitakazopatikana pindi mradi huo utakapokamilika kuwa ni pamoja na kutoa ajira kwa watumiaji wa tanuri hilo sambamba na Serikali kupata mapato kupitia biashara ya ukaushaji mbao hapa nchini.

Amesema mradi huo utakapokamilika na kuanza kutumika wafanyabiashara wa mbao watanufaika kwa kiasi kikubwa na kuwataka watengenezaji wa samani kutumia mbao zilizokauka ili kuondoa malalamiko ya wateja wao wanaolalamikia samani zao kuharibiwa na wadudu waharibifu.










PICHA NA TATYANA CELESTINE

Post a Comment

0 Comments