SUAMEDIA

Wananchi wahimizwa kutumia huduma za Vuyisile Mini Furniture Factory SUA

Na: Ngolo Mboje

Wananchi wamehimizwa kutumia huduma za Kiwanda cha Uchakataji Mbao cha Vuyisile Min Furniture Factory, kilichopo katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), kutokana na uwezo wake wa kuongeza thamani ya mazao ya misitu kupitia matumizi ya teknolojia za kisasa.

Akizungumza na SUA Media, Mhadhiri Msaidizi kutoka Idara ya Uhandisi Misitu na Sayansi za Mazao ya Misitu,  Ndaki ya Misitu, Wanyapori na Utalii Mbonea Joshua, amesema kiwanda hicho ni nyenzo muhimu katika uzalishaji wa bidhaa mbalimbali zenye thamani kubwa zinazotokana na miti na mbao.

Amesema kiwanda hicho kinatumia mashine za kisasa, ikiwemo Circular Saw kwa ajili ya kukatia mbao na Multiblade Saw kwa ajili ya kuchana mbao, ambazo hurahisisha kazi na kuongeza ufanisi katika uchakataji wa mazao ya misitu.

Ameongeza kuwa kiwanda hicho kina tanuru la kukaushia mbao laini na ngumu, ambalo huondoa unyevunyevu kwenye mbao mbichi na kuzifanya zidumu kwa muda mrefu kwa kupunguza madhara yanayoweza kusababishwa na wadudu pamoja na changamoto nyingine zinazotokana na unyevunyevu.

Joshua amesema kiwanda hicho pia kina mchango mkubwa katika shughuli za utafiti kwa kutengeneza sampuli za maabara zinazotumika katika tafiti mbalimbali, zikiwemo zinazohusu vifaa na mitambo. Ameeleza kuwa tafiti hizo zimechangia kupatikana kwa machapisho ya kisayansi yanayosaidia jamii kupata uelewa kuhusu matumizi bora ya teknolojia za uchakataji na uongezaji thamani wa mazao ya misitu.

Aidha, amesema kiwanda hicho ni kituo muhimu cha mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wa shahada ya kwanza, uzamili na uzamivu, hususan wanaosomea Sayansi ya Misitu pamoja na Sayansi ya Teknolojia ya Mbao na Uongezaji Thamani. Kupitia mafunzo hayo, wanafunzi hupata ujuzi wa kuchakata mazao ya misitu kuanzia gogo hadi bidhaa ya mwisho yenye thamani.

Bw. Joshua amewakaribisha wananchi kutembelea na kutumia huduma zinazotolewa na kiwanda hicho, akieleza kuwa shughuli zake zinafanyika kwa kuzingatia utunzaji wa mazingira.


Post a Comment

0 Comments