Na: Ngolo Mboje
Wanafunzi, wazazi na walezi wamehimizwa kujitokeza mapema
kufanya udahili katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), hususan katika
programu mpya zilizoanzishwa, ili kunufaika na mafunzo yanayolenga kuwajengea
wahitimu ujuzi wa vitendo unaohitajika katika soko la ajira.
Akizungumza na SUA Media katika banda la udahili la chuo hicho kwenye Maonesho ya Nanenane 2026, Afisa Udahili wa SUA, Bi. Grace Kihombo, amesema chuo kimejipanga kuendelea kutoa elimu inayozingatia zaidi mafunzo kwa vitendo kupitia programu mpya zilizoanzishwa mwaka 2026.
Amesema programu hizo zinalenga kuwaandaa wanafunzi kuwa na
maarifa, ujuzi na uwezo wa kujiajiri au kuajiriwa katika sekta mbalimbali baada
ya kuhitimu masomo yao.
Bi. Kihombo amezitaja programu hizo kuwa ni Shahada ya
Kilimo na Elimu (Bachelor of Agriculture with Education), Shahada ya Nguo,
Vitambaa na Mitindo ya Mavazi (Bachelor of Textiles and Fashion Studies),
Shahada ya Uhandisi wa Ujenzi (Bachelor of Civil Engineering), pamoja na
Shahada ya Usalama wa Mtandao na Uchunguzi wa Kidijitali (Bachelor of
Cybersecurity and Digital Forensics).
Amesema kuanzishwa kwa programu hizo ni sehemu ya jitihada za SUA za kupanua fursa za elimu ya juu na kukidhi mahitaji ya wataalamu katika maeneo ya teknolojia, viwanda, elimu na maendeleo ya uchumi wa taifa.
Aidha, Bi. Kihombo ameeleza kuwa SUA ni miongoni mwa vyuo
vinavyojikita katika utoaji wa mafunzo ya vitendo, hususan katika sekta za
kilimo, mifugo na maeneo mengine ya kitaaluma. Wanafunzi hupata nafasi ya
kujifunza kwa kutumia mashamba, mifugo, viwanda, maabara na miundombinu mingine
ya chuo, jambo linalowawezesha kupata uzoefu wa moja kwa moja kabla ya
kuhitimu.
Ameongeza kuwa udahili uko wazi kwa waombaji wote wenye
sifa, huku akiwasisitiza kufuata vigezo vilivyowekwa na kukamilisha mchakato wa
maombi mapema ili kuepuka changamoto zinazoweza kujitokeza wakati wa udahili.
Pia, amewashauri wazazi, walezi na wanafunzi ambao bado
hawajapata mwelekeo sahihi kuhusu programu zinazolingana na ufaulu wao
kutembelea banda la udahili la SUA katika Maonesho ya Nanenane, ambako watapata
ushauri wa kitaalamu utakaowasaidia kufanya maamuzi sahihi kuhusu uchaguzi wa
programu za masomo.
0 Comments