SUAMEDIA

Mafunzo ya Amali yawajengea wanafunzi wa Mafiga uwezo wa kujiajiri

 Na: Ngolo Mboje

Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Mafiga wamesema mafunzo ya amali yamewajengea uwezo wa kujifunza kwa vitendo, kutumia teknolojia za kisasa na kujiandaa kujiajiri kupitia shughuli za kilimo na ufugaji wenye tija kwa manufaa yao na jamii.

Wanafunzi hao akiwemo Maulidi Nyamoga na Husna Abdallah wameyasema hayo katika Maonesho ya Nanenane 2026, baada ya kupata fursa ya kuonesha na kueleza maarifa mbalimbali waliyopata kupitia mafunzo ya vitendo yanayotolewa kwa ushirikiano na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA).

Wamesema miongoni mwa teknolojia walizojifunza ni mfumo wa umwagiliaji kwa njia ya matone, unaosaidia kutumia maji kwa ufanisi kwa kuyapeleka moja kwa moja kwenye mizizi ya mimea. Mfumo huo husaidia kuhifadhi unyevunyevu wa udongo, kuimarisha ukuaji wa mimea na kuongeza uzalishaji wa mazao.

Aidha, wanafunzi hao wamesema mafunzo hayo yamewaongezea uelewa katika sekta ya mifugo, hususan kuhusu mbinu bora za utunzaji wa mifugo zinazolenga kuimarisha afya, lishe na uzalishaji wake.

Wameishukuru SUA kwa kuwapatia mafunzo ya vitendo pamoja na vifaa vya kujifunzia, wakisema elimu hiyo itawawezesha kujiajiri, kuwa wabunifu na kutumia maarifa waliyoyapata kuboresha shughuli za kilimo na ufugaji.

“Tunashukuru SUA kwa kutupatia mafunzo ya vitendo na vifaa vya kujifunzia. Elimu hii itatusaidia kujitengenezea ajira, kuwa wabunifu na kutumia teknolojia tulizojifunza katika kuboresha uzalishaji wa kilimo na mifugo,” wamesema wanafunzi hao.

Kwa upande wake, Mwalimu wa Somo la Afya ya Wanyama na Uzalishaji katika Shule ya Sekondari Mafiga, Isack Mwamba, amesema mafunzo ya amali yanawajengea wanafunzi uwezo wa kujiajiri baada ya kuhitimu masomo yao, pamoja na kuwa mabalozi wa kuelimisha jamii kuhusu matumizi ya teknolojia za kisasa katika kilimo na ufugaji.

Mwamba amesema ushirikiano kati ya Shule ya Sekondari Mafiga na SUA ni hatua muhimu katika kuimarisha utekelezaji wa sera ya elimu ya amali, inayolenga kuwaandaa wanafunzi kujitegemea na kushiriki kikamilifu katika maendeleo ya sekta za kilimo na mifugo nchini.

Ameishukuru menejimenti ya SUA kwa kuendelea kutoa mafunzo hayo kwa wanafunzi wa Mafiga Sekondari, akisema yamekuwa na mchango mkubwa katika kuwapatia ujuzi wa vitendo unaowaandaa kwa maisha, kujiajiri na kushindana katika soko la ajira.

Post a Comment

0 Comments