SUAMEDIA

Prof. Mkenda afungua Maonesho ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu Tanga

 Na: Mwandishi wetu

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Mhe. Prof. Adolf Mkenda, Agosti 18, 2026, amefungua rasmi Maonesho ya Wiki ya Kitaifa ya Elimu, Ujuzi na Ubunifu yanayofanyika katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagara, Jijini Tanga.

Maonesho hayo yamezikutanisha taasisi mbalimbali zinazotoa huduma katika sekta za elimu, sayansi na teknolojia, pamoja na ujuzi na ubunifu, yakitoa fursa kwa wananchi na wadau kupata taarifa, maarifa na huduma mbalimbali moja kwa moja kutoka kwa wataalamu wa taasisi zinazoshiriki.

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ni miongoni mwa taasisi zinazoshiriki maonesho hayo, ikiwa ni sehemu ya jitihada zake za kuwafikia wananchi na wadau, kuwaelimisha kuhusu programu zinazotolewa na chuo, pamoja na huduma na fursa mbalimbali zinazotolewa kwa jamii.

Maonesho hayo yanafanyika chini ya kauli mbiu, “Elimu, Ujuzi na Ubunifu ni Njia ya Kufikia Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050,” inayosisitiza nafasi muhimu ya elimu, ujuzi na ubunifu katika kujenga rasilimaliwatu yenye maarifa, ujuzi na uwezo wa kuchangia kikamilifu katika maendeleo ya Taifa.

Hafla ya ufunguzi imehudhuriwa na viongozi mbalimbali kutoka taasisi za umma, wakiwemo viongozi wa SUA wakiongozwa na Prof. Maulid Mwatawala, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu.

Wananchi na wadau wa elimu wanakaribishwa kutembelea banda la SUA katika maonesho hayo na kupata taarifa kuhusu programu za masomo, tafiti, ubunifu, pamoja na huduma mbalimbali zinazotolewa na Chuo kwa manufaa ya jamii.




Post a Comment

0 Comments