SUAMEDIA

Wanafunzi SUA waonesha ubunifu wa mavazi katika Maonesho ya Mafunzo kwa Vitendo

 Na: Farida Mkongwe

Wanafunzi wa Shahada ya Sayansi ya Familia na Mlaji kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wameonesha ubunifu wao katika kubuni na kushona mavazi kupitia maonesho ya mafunzo kwa vitendo ambayo yamelenga  kuwaandaa wanafunzi hao kuingia katika soko la ajira na kujiajiri baada ya kuhitimu masomo yao.



Akifungua Maonesho hayo kwa niaba ya Mkuu wa Idara ya Lishe na Stadi za Mlaji yaliyofanyika Julai 17, 2026 chuoni hapo, Dkt. Safiness Msollo amesema maonesho hayo ni sehemu muhimu ya mtaala wa kozi hiyo kwani yanawapa wanafunzi nafasi ya kuonesha maarifa na ujuzi walioupata darasani kwa vitendo na kwamba yanawajengea uwezo wa kujiajiri au kuajiriwa katika sekta mbalimbali mara baada ya kuhitimu.

Naye Mhadhiri kutoka Idara hiyo, Dkt. Zahra Majili, amesema lengo kuu la maonesho hayo ni kuwapa wanafunzi fursa ya kubuni na kutengeneza mavazi yatakayowasilishwa kwa watumiaji ili kupata maoni yatakayoboresha kazi hizo. 

Amefafanua kuwa shughuli hiyo ni sehemu ya tathmini ya masomo, ambapo wanafunzi hupata alama kulingana na kiwango cha ubunifu, ubora wa kazi na namna wanavyowasilisha bidhaa zao. Aidha, amewahimiza wanafunzi kutumia maarifa wanayopata chuoni katika maisha yao ya kila siku.


Kwa upande wake, Mwalimu Mary Marcel ambaye hufundisha masomo ya ushonaji wa nguo na ubunifu wa mavazi, amesema wanafunzi wengi wameonesha kiwango kikubwa cha ubunifu katika kushona na kubuni mavazi, pamoja na kuzingatia kanuni za uvaaji, uchanganyaji wa rangi na aina ya mavazi yanayofaa kwa matukio mbalimbali.

Amesema wahitimu wengi wa programu hiyo tayari wamejiajiri, huku wengine wakitumia mitandao ya kijamii kufundisha masuala ya mitindo na ubunifu wa mavazi, na kuwashauri wanafunzi kutanguliza fikra za kujiajiri badala ya kusubiri ajira.


Baadhi ya wanafunzi walioshiriki maonesho hayo, akiwemo Beatrice Marya wa mwaka wa tatu na Barton Shoo wa mwaka wa pili wa Shahada ya Sayansi ya Familia na Mlaji, wamesema maonesho hayo yamewapa nafasi ya kuingia katika ulimwengu wa kazi na biashara kwa kuwakutanisha na wadau mbalimbali, wakiwemo waajiri na wateja watarajiwa.

Wamesema kupitia maonesho hayo wameweza kuonesha uwezo wao wa kubuni, kushona, kuchagua vitambaa vinavyofaa na kuwasilisha bidhaa zenye ubora zinazokidhi mahitaji ya jamii na soko la ajira.








Post a Comment

0 Comments