SUAMEDIA

Kafulila: Maarifa na PPP Vichocheo Vikuu vya Mpango wa Nne wa Taifa wa maendeleo wa miaka mitano

 Na: Calvin Gwabara – Morogoro.

Imeelezwa kuwa Ubia kati ya Serikali na Sekta Binafsi (PPP),Weledi wa watu kwenye usimamizi wa miradi na Taasisi pamoja na maarifa kwenye sekta za uzalishaji na utoaji huduma ndio nguzo inayoweza kuifanya Tanzania kufikia malengo ya Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP IV) wa kipindi cha 2026/27–2030/31.

Mkurugenzi Mtendaji wa kituo cha Ubia kati ya Serikali na Sekta binafsi (PPPC) Bwana David Kafulila wakati akitoa mhadhara katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi Mtendaji wa kituo cha Ubia kati ya Serikali na Sekta binafsi (PPPC) Bwana David Kafulila wakati akitoa mhadhara wa wazi kwenye Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo kuhusu nafasi ya ushirikiano kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi katika kuleta mageuzi ya kilimo kwa muktadha wa malengo ya Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP IV) wa kipindi cha 2026/27–2030/31.

Amesema malengo ya PPP ni kuvuta mitaji ya sekta binafsi kwa kuipa nafasi ya kuwekeza kwenye miradi na utoaji wa huduma,kuongeza matumizi makubwa ya teknolojia na ubunifu kwakuwa sekta binafsi zina nafasi kubwa katika kutumia teknolojia kwa haraka pamoja na kuwa na weledi katika kusimamia makampuni na miradi inayokabidhiwa ili kuongeza ufanisi na tija kwao.

“Duniani huko hasa nchi zilizoendelea zinashindana kwa ubora wa watu wake katika kufanya kazi na matumizi ya teknolojia za juu katika kutoa huduma, kuongeza ufanisi na kuleta faida, jambo hili linakwenda sambamba na kuhakikisha watu wake wanakuwa na maarifa na lishe lakini nchi hizo zikihimiza swala la ubia kati ya sekta ya Umma na sekta binafsi ili kuchochea maendeleo” alieleza Kafulila.

Mkurugenzi huyo wa PPPC amesema swala la PPP sio jambo la Tanzania bali ndio agenda ya dunia na nchi zilizoendelea na katika miaka mitano tangu kuanzishwa kwa Ubio huo hapa nchini, Tanzania imeweza kukuza thamni yake kutoka Trilioni 2 hadi kufikia zaidi ya 8 jambo ambalo limechangiwa na serikali kufungua milango kwa sekta binafsi kushirikiana na sekta ya umma.

Aidha bwana Kafulila amesema PPP inatoa fursa kwa sekta binafasi kufanya shughuli mbalimbali za kibiashara na kiuchumi ambazo zinatakiwa kufanywa na serikali ili yenyewe ibaki na zile za kihuduma zaidi ambazo sekta binafsi haiwezi kutokana na kutokuwa na faida sana na kwa kufanya hivyo serikali inajipunguzia mzigo huku nchi ikipata maendeleo.

Amesema Chuo Kikuu cha Sokoine kina mchango mkubwa katika kusaidia eneo la maarifa hasa ikizingatiwa kuwa sekta hiyo inachangia ajira kwa wananchi kwa zaidi ya asilimia 65 huku asilimia 70 ya watanzania wanaishi vijijini hivyo bila kuwa na wataalamu wa kutosha ni vigumu kuongeza tija kwenye sekta hiyo na kapambana na umasikini.

Awali akizungumza kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo Prof. Raphael Chibunda kabla ya kumkaribisha kuongea na wanajumuiya ya SUA, Naibu Mkamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Mipango fedha na Utawala Prof. Amandus Muhairwa amesema Chuo hicho kinashiriki kwa asilimia kubwa katika kutekeleza mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa kuchangia katika kuzalisha wataalamu, Kufanya tafiti na kutoa ushauri wa kitaalamu katika sekta mbalimbali zinazohusiana na kilimo na sayansi za kilimo.

Naibu Mkamu mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Mipango fedha na Utawala Prof. Amandus Muhairwa akizungumza kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi kutoa mhadhara.

“Uamuzi wa PPPC kufanya mhadhara huu chuoni hapa haukuja kwa bahati mbaya bali ni kutokana na kituo hicho kutambua nafasi ya SUA katika kutekeleza Mpango huo wa maendeleo na katika nafasi yake ya kuzalisha wataalamu hodari na mahiri wanye mchango mkubwa katika kukuza sekta ya Umma na sekta binafsi kwa kuzalisha ajira na kuleta maendeleo ya watu” Alibainisha Muhairwa.

Aliongeza “Nchi zilizoendelea sana kama China zimetumia sana Elimu, Tafiti. Ubunifu, Kilimo na Teknolojia katika kujenga uchumi imara hali ambayo inasaidia kuongeza tija katika uzalishaji wa bidhaa na teknolojia mbalimbali kwani serikali inatoa miongozo na sera huku sekta binafsi ikitoa mitaji na teknolojia”.

Prof. Muhairwa amesema Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo SUA kipo tayari na kinaendelea kusaidia utekelezaji wa Mpango wa Nne wa Taifa wa Maendeleo wa Miaka Mitano (FYDP IV) wa kipindi cha 2026/27–2030/31 kupitia kuleta mageuzi ya sekta ya Kilimo.

Akitoa shukrani Rasi wa Ndaki ya Kilimo Dkt. Nyambilila Amuri amesema Mhadhara huo umeleta faida kubwa kwa wanajumuiya wa SUA kwa kukutanisha Watafiti,Walimu, Wanafunzi na wadau wengine hasa katika kuelewa dhana nzima za PPP kwa kina na kutoa nafasi ya kuuliza maswali mbalimbali ambayo yamesaidia wanazuoni hao kuona nafasi yao katika kutekeleza mpango huo wa maendeleo ya Taifa kupitia PPP.

“Sote tutakubaliana kuwa wasilisho la Mkurugenzi wa PPPC limegusa kila kozi zinazofundshwa hapa chuoni hivyo kila mmoja anaweza kusoma akijitazama nafasi yake kwenye kushiriki kwenye mpango huu wa nne wa taifa kupitia maarifa anayoyapata chuoni hapa, hivyo tujipange mapema kuwaza namna ya kushiriki uwekezaji wa ubia na serikali kwenye nyanja mbalimbali” Alisema Dkt. Amuri.

MATUKIO KATIKA PICHA WASHIRIKI WA MHADHARA HUO WAKIFUATILIA NA KUULIZA MASWALI.


 











Post a Comment

0 Comments