SUAMEDIA

SUA yahimiza ubunifu kutatua changamoto za jamii

 Na: Ngolo Mboje

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kusisitiza umuhimu wa ubunifu na matumizi ya maarifa ya vitendo kwa wanafunzi ili kuwawezesha kubuni suluhisho la changamoto mbalimbali za kijamii na kuchangia maendeleo ya taifa.

 Rasi wa Ndaki ya Misitu, Wanyamapori na Utalii, SUA, Prof. Agnes Sirima akizungumza na washiriki

Akizungumza chuoni hapo Juni 25/2026  kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Rasi wa Ndaki ya Misitu, Wanyamapori na Utalii, SUA, Prof. Agnes Sirima, amesema chuo kinaendelea kuhimiza wanafunzi kutumia maarifa wanayoyapata darasani na katika mafunzo ya vitendo kuibua bunifu zitakazoongeza thamani ya bidhaa na huduma, kukuza ajira na kuchangia maendeleo ya jamii.

Amesema ubunifu unaofanywa na wanafunzi hauwanufaishi wao pekee, bali una mchango mkubwa katika kutatua changamoto za jamii na kuharakisha maendeleo ya kiuchumi ya nchi. Aidha, amewataka wanafunzi kuendelea kutumia fursa wanazozipata chuoni kukuza uwezo wao wa ubunifu na ujasiriamali.

 Rasi wa Ndaki ya Misitu, Wanyamapori na Utalii, SUA, Prof. Agnes Sirima akisikiliza maelezo kutoka kwa Magoti Ernest, mmoja wa wanufaika wa SUA Innovation Hub


Kwa upande wake, Mratibu wa Kituo cha Ubunifu ‘SUA Inovation Hub’ SUA, Dkt. Doreen Ndossi, amesema kituo hicho kinaendelea kuwa jukwaa la kulea na kuendeleza wabunifu kwa kuwapatia mafunzo, ushauri wa kitaalamu na kuwaunganisha na fursa mbalimbali zitakazowawezesha kukuza bunifu zao.

Dkt. Ndossi amewapongeza wabunifu walioshiriki katika maonesho hayo kwa kuonesha uwezo mkubwa wa kutumia ubunifu na teknolojia kutatua changamoto mbalimbali, huku akiwahimiza wanafunzi na vijana wengine kujitokeza kushirikiana na Sua  Innovation Hub ili kupata mwongozo na msaada wa kitaalamu utakaowawezesha kubadilisha mawazo yao kuwa bidhaa na huduma zenye manufaa kwa jamii.

Mratibu wa Kituo cha Ubunifu ‘SUA Inovation Hub’ SUA, Dkt. Doreen Ndossi akitoa maelezo juu ya Inovation Hub


Kwa upande wake,Ndg. Magoti Ernest, mmoja wa wanufaika wa SUA Innovation Hub na mlezi wa wabunifu, amesema mafanikio aliyoyapata yametokana na malezi na ushauri alioupata alipokuwa mwanafunzi chuoni hapo.

Magoti amewataka watumishi wa chuo kuendelea kuwaunga mkono wanafunzi wenye mawazo bunifu ili yaweze kugeuka kuwa teknolojia na biashara zinazoweza kutatua changamoto za jamii.

Amesema mafanikio hayo yanaonesha uwezo mkubwa wa wanafunzi wa Sua  katika ubunifu na kwamba, kwa kuendelea kupata ushauri na mazingira rafiki ya kujifunza, wanaweza kufanya vizuri zaidi katika ngazi ya kitaifa na kimataifa.



Post a Comment

0 Comments