SUAMEDIA

Diwani Mstaafu Mbeya apongeza elimu ya SUA katika kupambana na homa ya kiwele

 Na: Ayoub Mwigune 

 Diwani mstaafu na mfugaji wa ng’ombe wa maziwa, Johnson Kuruwa Mwamdengo kutoka Wilaya ya Rungwe mkoani Mbeya, amepongeza juhudi za watafiti na wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa kuendelea kuwafikia wafugaji mashambani na kuwapatia elimu ya kitaalamu inayolenga kuboresha ufugaji.

Akizungumza baada ya kutembelewa na wataalamu hao, Mwamdengo amesema elimu inayotolewa na SUA imechangia kwa kiasi kikubwa kupunguza changamoto ya homa ya kiwele kwa ng’ombe wa maziwa, pamoja na kuboresha uzalishaji na ubora wa maziwa.

Amesema mafunzo kuhusu usafi wa mabanda, ukamuaji sahihi na udhibiti wa magonjwa ya mifugo yamewasaidia wafugaji wengi kuimarisha afya ya ng’ombe wao na kuongeza tija katika uzalishaji wa maziwa.

Mwamdengo amesema maeneo mengi ya Mkoa wa Mbeya hukumbwa na mvua za muda mrefu, hali inayosababisha mabanda kuwa na unyevunyevu unaoweza kuchochea maambukizi ya homa ya kiwele. Amesema elimu kutoka kwa wataalamu imekuwa na mchango mkubwa katika kuwawezesha wafugaji kukabiliana na changamoto hiyo.

“Tunazipongeza tafiti hizi zinazoendelea, na tunaamini zitatoa suluhisho zaidi kwa changamoto hii ili kuwasaidia wafugaji kuongeza uzalishaji na ubora wa maziwa yanayopelekwa sokoni,” amesema Mwamdengo.

Aidha, amesema mafunzo kuhusu lishe bora ya mifugo yamewasaidia wafugaji kutumia vizuri rasilimali zinazopatikana katika maeneo yao, ikiwemo majani, mabua ya migomba na virutubisho vingine, jambo lililochangia kuimarisha afya ya mifugo na kuongeza uzalishaji wa maziwa.

Mwamdengo amesema kuendelea kwa ushirikiano kati ya watafiti wa SUA na wafugaji kutasaidia kutatua changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika sekta ya mifugo, na hivyo kuongeza mchango wa sekta hiyo katika uchumi wa wananchi na taifa kwa ujumla.




Post a Comment

0 Comments