Na: Vumilia Kondo
Ufugaji
wa nguruwe ni miongoni mwa miradi inayokua kwa kasi nchini kutokana na uwezo wake wa kuinua kipato cha
kaya kwa muda mfupi.
Hata hivyo, changamoto za magonjwa, lishe duni, ukosefu wa elimu ya kitaalamu na masoko zimekuwa zikirudisha nyuma juhudi za wafugaji wengi.
Ili
kukabiliana na changamoto hizo, Taasisi ya Elimu ya Kujiendeleza (ICE) ya Chuo
Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), imeendesha mafunzo maalum ya ufugaji bora
wa nguruwe yaliyowaleta pamoja wataalamu, wafugaji wenye uzoefu pamoja na watu
wanaotarajia kuanza mradi huo kutoka mikoa nane nchini Tanzania.
Akizungumza
wakati wa mafunzo hayo kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha
Kilimo, Prof. Raphael Chibunda, Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Kujiendeleza
SUA, Dkt. Devotha Mosha, amesema ufugaji wa nguruwe una nafasi kubwa katika
kuinua kipato cha kaya na kuchangia usalama wa chakula, hivyo ni muhimu
wafugaji kupata elimu ya msingi kabla ya kuanza shughuli hiyo.
“Tunashauri
wafugaji wa nguruwe, kuku na sungura kupata mafunzo ya msingi kabla ya kuanza,hii
inawasaidia kufikia malengo ya kukuza kipato na kuimarisha usalama wa chakula,”
amesema Dkt. Mosha.
Kwa upande wake, mtaalamu wa mifugo kutoka SUA, Prof. Faustine Lekule, amesema sekta ya ufugaji wa nguruwe inakabiliwa na changamoto kuu nne ambazo ni magonjwa, hasa yasiyo na tiba kama homa ya nguruwe ya Afrika, gharama na ubora wa chakula, ukosefu wa elimu kwa wafugaji pamoja na changamoto za masoko.
Amesema
mafunzo hayo yanalenga kuwapa washiriki uelewa wa kina kuhusu mbinu bora za
ufugaji kuanzia lishe, uzalishaji, udhibiti wa magonjwa hadi usimamizi wa
shamba, ili waweze kufuga kwa tija na kupata faida.
“Mafunzo
haya yanalenga kuwapa washiriki uelewa wa kina wa mbinu bora za ufugaji kuanzia
lishe, uzalishaji hadi usimamizi wa shamba, mambo ambayo yatawasaidia kuona
faida za ufugaji wa nguruwe,” amesema Prof. Lekule.
Baadhi
ya washiriki wa mafunzo hayo wamesema elimu waliyoipata imewapa mwanga mpya
kuhusu namna bora ya kuendesha ufugaji wa nguruwe kwa kuzingatia kanuni za
kitaalamu.
Mmoja
wa washiriki hao, Anastasia Seleli, amesema ingawa bado hajaanza kufuga,
ameamua kushiriki mafunzo hayo ili ajipange vizuri kabla ya kuingia kwenye
biashara hiyo.
“Nilikuwa na mambo machache kichwani, lakini hapa napata mengi zaidi ya niliyoyatarajia. Mafunzo haya ni mkombozi kwangu kwa sababu yananisaidia kujua namna ya kuanza kwa usahihi,” amesema Anastasia.
Naye
Blasius Kigeso kutoka Dodoma amesema aliamua kushiriki mafunzo hayo kutokana na
changamoto za magonjwa pamoja na ukosefu wa ujuzi sahihi miongoni mwa wafugaji
wengi.
“Wafugaji
wengi hutegemea uzoefu wa kawaida bila msingi wa kitaalamu. Elimu ninayopata
itanisaidia kupunguza hasara na kuongeza tija katika shughuli zangu,” amesema
Blasius.
Kwa
ujumla, mafunzo hayo yanatoa nafasi kwa washiriki kujifunza mbinu za kisasa za
ufugaji, ikiwemo uchaguzi wa mbegu bora za nguruwe, uzalishaji kwa njia ya
kisasa kama uhimilishaji, pamoja na matumizi ya teknolojia kama kamera katika
kusimamia mifugo.
Mbinu
hizo zinatajwa kuwa na mchango mkubwa katika kuongeza ubora wa nyama, kasi ya
ukuaji wa mifugo na tija kwa ujumla.
Kupitia
mafunzo hayo, SUA imeendelea kusisitiza umuhimu wa wafugaji kupata elimu ya
kitaalamu ili kuhakikisha ufugaji unakuwa endelevu, wenye tija na wenye manufaa
kwa kaya na taifa kwa ujumla.





0 Comments