Na : Ayoub Mwigune - Gairo
Mkuu wa Mkoa wa
Morogoro amewahimiza wafanyakazi kufanya kazi kwa staha, kujituma na kuzingatia
maadili ya kazi ili kuchangia kikamilifu katika kufikia Dira ya Maendeleo ya
Taifa 2050.
Ameyasema hayo wakati
wa maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi, 2026) yaliyofanyika
kimkoa katika Wilaya ya Gairo, mkoani Morogoro.
Akizungumza katika
hafla hiyo, amesema Tanzania ni nchi yenye malengo makubwa ya maendeleo, na
mafanikio yanayoendelea kupatikana ni matokeo ya uongozi thabiti wa Serikali
pamoja na ushirikiano mzuri kati ya Serikali na vyama vya wafanyakazi.
Aidha, amewahimiza wananchi kufuatilia taarifa
za habari ili kufahamu changamoto zinazoikabili nchi yao na namna ya kushiriki
katika kuzitatua.
Amesisitiza kuwa Serikali
ipo karibu na wafanyakazi na iko tayari kupokea na kushughulikia changamoto zao
na kuwa baadhi ya madai ya wafanyakazi tayari yamepatiwa ufumbuzi, huku mengine
yakiendelea kufanyiwa kazi, kwani changamoto hizo haziwezi kumalizika kwa
wakati mmoja bali zinahitaji juhudi endelevu.
Kuhusu maslahi ya
wafanyakazi, amesema nyongeza ya mishahara huzingatia vigezo mbalimbali ikiwemo
pato la taifa. Aidha, amewataka waajiri kuhakikisha wanalipa madeni ya
wafanyakazi, hususan wastaafu, na kusisitiza matumizi ya njia za upatanishi
katika kutatua migogoro ya kikazi ili kudumisha amani na utulivu mahali pa
kazi.
Kwa upande wake,
Mwenyekiti wa TUCTA Mkoa wa Morogoro, Bw. Elius Yuda Mtungirwa, amesema
wafanyakazi wataendelea kuwa wabunifu, kujituma na kuzingatia kanuni na
miongozo ya kazi huku wakidumisha amani na mshikamano.
Kwa upande wa Chuo
Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), wafanyakazi hodari wa mwaka 2026, Bw.
Kajura Magoma na Dkt. Nkuba Mbeho, wamesema mafanikio yao yametokana na
kujituma kazini, kutimiza majukumu kwa ufanisi na kujenga nidhamu ya kazi,
pamoja na uwezo wa kukabiliana na changamoto katika maeneo yao ya kazi.


0 Comments