Na: Ngolo Mboje- Morogoro.
Watumishi
wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wamehimizwa kufanya kazi kwa bidii,
kuimarisha utendaji wao na kuchangia kwa dhati maendeleo ya chuo pamoja na
jamii kwa ujumla.
Wito
huo umetolewa na Prof. Amandus Muhairwa, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa
Mipango, Fedha na Utawala, kwa niaba ya Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Raphael
Chibunda, wakati wa Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani (Mei Mosi, 2026)
yaliyofanyika katika Kampasi ya Edward Moringe, mkoani Morogoro.
Akizungumza
katika hafla hiyo, Prof. Muhairwa amebainisha kuwa SUA ni Taasisi ya mfano
katika tafiti bunifu na utoaji wa huduma kwa jamii na kwamba Chuo hicho kina
mazingira rafiki ya kazi, mifumo inayozingatia haki, uwazi na uwajibikaji,
ambayo ni msingi muhimu wa kujenga taasisi yenye ushindani na mchango halisi
katika maendeleo ya jamii.
Aidha,
ameishukuru Serikali kwa kuipatia SUA ajira mpya 263, hatua ambayo imeongeza
nguvu kazi chuoni hapo, ameongeza kuwa chuo kinaendelea kuboresha upatikanaji
wa vifaa vya kazi na kuimarisha mifumo ya ununuzi ili kuongeza ufanisi na
kuendeleza dhamira ya pamoja ya kujenga SUA iliyo bora zaidi.
Katika
hatua nyingine, Prof. Muhairwa amewapongeza wafanyakazi wote, hususan
waliotunukiwa tuzo mbalimbali, kwa juhudi na kujituma kwao katika kutekeleza
majukumu yao ya kila siku na kusema mchango wao umeiwezesha SUA kuendelea kuwa
kitovu muhimu cha elimu ya kilimo nchini.
Kwa
upande wao, Mwenyekiti wa RAAWU tawi la SUA, Bw. Faraja Kamendu, pamoja na
Mwenyekiti wa THTU tawi hilo, Bw. Nikson Mkiramwene, wameipongeza Menejimenti
ya Chuo na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutambua mchango wa
wafanyakazi na kushughulikia baadhi ya changamoto, ikiwemo ulipaji wa deni la
wanataaluma na huduma za matibabu kwa wafanyakazi wa SUA.
Naye,
Prof. Herzon Nonga, akitoa shukrani kwa niaba ya wafanyakazi bora, ameushukuru
uongozi wa SUA kwa kutambua juhudi zao kupitia utoaji wa tuzo, na kuwataka
wafanyakazi wote kuendelea kufanya kazi kwa bidii kwa ajili ya mustakabali na
maendeleo ya chuo.
Maadhimisho
ya Siku ya Wafanyakazi Duniani hufanyika kila mwaka tarehe 1 Mei, yakilenga
kutambua mchango wa wafanyakazi katika maendeleo ya jamii na Taifa kwa ujumla.
0 Comments