SUAMEDIA

Mapinduzi ya Kilimo: SUA na AgriMazao Wapiga Msasa Wanafunzi Matumizi ya Droni Morogoro

 Na: Vumilia Kondo

Chuo Kikuu cha Kilimo cha Sokoine (SUA) kimepiga hatua nyingine kubwa katika kuandaa wataalamu wa kilimo cha kisasa baada ya kuendesha mafunzo ya vitendo ya teknolojia ya ndege nyuki (droni) kwa wanafunzi wote wanaosomea fani mbalimbali za kilimo na ufugaji.


Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Raphael Chibunda akizungumza na wanafunzi (hawako pichani) kushoto ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Mipango, Utawala na Fedha Prof. Amandus Muhairwa

Mafunzo hayo yamefanyika kwa lengo la kuwapa vijana ujuzi wa jinsi ndege nyuki zinavyoweza kutumika kupulizia viuadudu, kufanya tathmini ya afya ya mazao, na ramani za kidijitali za mashamba.

Makamu Mkuu wa Chuo, Profesa Raphael Chibunda, akizungumzia uzito wa mafunzo hayo, amebainisha kuwa chuo kimefanya maamuzi ya makusudi kuwekeza kwenye teknolojia hiyo ili kuendana na dira ya Serikali ya Awamu ya Sita.

Wanafunzi wakishiriki mafunzo ya kurusha ndege nyuki

"Tumetenga bajeti kwa ajili ya kukuboresha jinsi tunavyofundisha wanafunzi wetu. Sisi kama wafundishaji hatuwezi kubaki nyuma, yaani tukaacha wahitimu wetu wakaenda kuona hivi vitu wanapokuwa wamemaliza chuo. Tumejipanga ili wawe waajiriwa bora, lakini sehemu kubwa wawe na ujuzi wa kwenda kujiajiri," amesema Profesa Chibunda.

Naye Rasi wa Ndaki ya Kilimo, Dokta Nyambilila Amuri akifafanua kiufundi kuhusu umuhimu wa mafunzo hayo, amesema matumizi ya droni ni sehemu ya utekelezaji wa mitahala mipya inayolenga kilimo cha uhakika (Precision Agriculture).

 Rasi wa Ndaki ya Kilimo, Dokta Nyambilila Amuri akizungumza na mwandishi wa SUA Media

"Matumizi ya droni yanaleta kilimo cha uhakika (precision agriculture). Tutaweza kutumia mbolea na viuatilifu kwa kiwango sahihi na kwa eneo sahihi, jambo linaloongeza tija na ufanisi wa pembejeo, huku tukikabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi kwa kufanya kilimo kiwe rafiki kwa mazingira."

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa  kampuni ya Agri Mazao Mohamedi Salimu, ameeleza kuwa ushirikiano wao na SUA unalenga kuwapa wanafunzi uzoefu wa vitendo kutoka sokoni.

  Ndege nyuki ikiwa angani

 Amebainisha kuwa droni zina uwezo wa kufanya kazi kubwa kwa muda mfupi, jambo ambalo ni mkombozi kwa mkulima katika kupunguza gharama za vibarua na dawa.

Wanafunzi walioshiriki mafunzo hayo akiwemo Elizabeth  Salim anayesomea uzalishaji na usimamizi wa mazao wameeleza namna teknolojia hiyo inavyobadilisha mtazamo wao wa kilimo.

"Zamani tulikuwa tunaangalia matatizo ya shambani kwa macho, lakini sasa hivi droni inatusaidia kuditekti (detect) matatizo na kurahisisha kazi ya kupulizia magugu na wadudu kwenye mahindi, jambo ambalo linapunguza gharama za uzalishaji."Amesema Elizabeth

Naye mwanafunzi Frankie Daudi ameongeza kuwa droni inasaidia kufanya 'mapping' ya eneo lote la shamba kwa muda mfupi na kwa usahihi wa hali ya juu ikilinganishwa na njia za kawaida.

Tukio hili linaashiria mwanzo wa msimu mpya wa mafunzo ambapo SUA imejipanga kuhakikisha teknolojia inakuwa nguzo kuu ya kilimo, ikiendana na kaulimbiu ya chuo hicho kuwa "Ardhi ni Hazina."





Post a Comment

0 Comments