Na: Calvin Gwabara – Dar es salaam.
Tanzania imeibuka kuwa kinara
barani Afrika katika matumizi ya teknolojia ya vinasaba (DNA) kukabiliana na
wadudu na magonjwa ya mazao.
![]() |
| Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Afya ya Mimea na Viuatilifu Tanzania (TPHPA) Prof. Joseph Ndunguru akionesha kifaa hicho cha kisasa cha utambuzi wa magonjwa na wadudu papohapo. |
Akizungumza katika mkutano wa
wadau wa bioteknolojia (BST) Prof. Joseph Canisius Ndunguru, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya afya
ya mimea na viuatilifu Tanzania (TPHPA), amesema hatua hiyo ni mapinduzi ya
kisayansi yanayobadilisha usimamizi wa afya ya mimea na usalama wa chakula
nchini.
“TPHPA ilianzishwa chini ya
Sheria ya Afya ya Mimea Na. 4 ya mwaka 2020 kwa lengo la kuimarisha usimamizi
wa afya ya mimea na viuatilifu na lengo lilikuwa kuunda mfumo madhubuti wa
kisheria na kisayansi unaolinda wakulima, walaji na maslahi ya biashara ya
kimataifa.Alibainisha Prof. Ndunguru.
Amesema miongoni mwa wadudu
hatari ni viwavijeshi vamizi anayejulikana kama funza wa majani ya Mahindi
(Fall Armyworm), ambaye amesababisha hasara kubwa ya mazao barani Afrika ambapo
katika baadhi ya maeneo, wakulima wamepoteza hadi asilimia 60 ya mavuno.
Alieleza kuwa wakulima wengi
hulazimika kunyunyiza viuatilifu mara kwa mara na kuchanganya kemikali kadhaa
lakini unyunyiziaji holela si suluhisho na unaongeza hatari za kiafya na
kuharibu mazingira.
Prof. Ndunguru amebainisha kuwa Ili
kukabiliana na changamoto hiyo, TPHPA imeanza kutumia vifaa vya kubebeka vya
uchunguzi wa DNA vinavyoweza kubaini aina halisi ya mdudu au kisababishi cha
ugonjwa shambani.
“Tanzania imekuwa nchi ya kwanza duniani
kutumia teknolojia hii katika sekta ya kilimo kwa kiwango cha kitaifa,” alisema
Prof. Ndunguru.
Aidha Mkurugenzi huyo mkuu wa
TPHPA amesema Teknolojia hiyo ilithibitika wakati wa uvamizi wa nzige katika
Wilaya ya Mpwapwa. Uchunguzi wa DNA ulithibitisha kuwa walikuwa Anacridium
incisum badala ya nzige wekundu waliokuwa wakihofiwa na hivyo
uUtambuzi sahihi uliwezesha kutumia dawa maalumu na kudhibiti uvamizi huo kwa
mafanikio.
Akieleza eneo lingine ambalo vifaa
hivyo vimetumika amesema ni wilaya ya Kilolo, uchunguzi wa kina ulibaini uwepo
wa vimelea mbalimbali vilivyoathiri nyanya na vitunguu kwa wakati mmoja na kugundua
kuwa mazao yalikuwa yanashambuliwa na mtandao wa magonjwa unaohusisha fangasi,
bakteria na virusi kwa pamoja.
“Teknolojia hii pia imeimarisha
biashara ya kimataifa kwani baada ya Umoja wa Ulaya kuhitaji uthibitisho kuwa
Tanzania haina bakteria hatari wa Xylella, TPHPA ilifanya maelfu ya vipimo vya
maabara, na hivyo kutokana na ripoti yetu ya kisayansi, Tanzania iliendelea
kuruhusiwa kufanya biashara na EU,” alieleza Mkurugenzi huyo Mkuu wa TPHPA
Prof. Ndunguru.
Mbali na hilo, TPHPA imewekeza
katika maabara za kisasa zenye uwezo wa kuchambua sampuli 2,000 za viuatilifu
kwa wiki kwani dhibiti unaotegemea sayansi unahakikisha wakulima wanapata viuatilifu
salama na sahihi kwani dhamira ya TPHPA ni kujenga mfumo wa kilimo endelevu na
himilivu. Bioteknolojia si anasa bali ni hitaji la msingi kwa mustakabali wa
usalama wa chakula.


0 Comments