SUAMEDIA

Bioteknolojia kuivusha Tanzania kwenye mapinduzi ya kilimo na ajira

 Na: Calvin Gwabara – Dar es salaam.

Serikali imetangaza kuwa bioteknolojia itakuwa mhimili mkuu wa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050, kwa lengo la kuongeza usalama wa chakula, ajira na ushindani wa uchumi wa Tanzania.

Naibu katibu Mkuu wizara ya Kilimo anayeshughulikia maendeleao ya mazao na usala wa chakula Prof. Peter Msoffe akiangalia sehemu ya maonesho ya bidhaa zinazozalishwa kwa kutumia teknolojia ya bioteknolojia .nje ya mkutano huo.

Akizungumza Dar es Salaam wakati wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Bioteknolojia Tanzania (BST),Naibu katibu Mkuu wizara ya Kilimo anayeshughulikia maendeleao ya mazao na usala wa chakula Prof. Peter Msoffe kwa niaba ya Waziri wa Kilimo  Mhe. Daniel Chongolo alisema teknolojia hiyo itawezesha uzalishaji wa mazao yanayostahimili mabadiliko ya tabianchi, kuongeza tija mashambani na kusaidia mapinduzi ya viwanda na afya.

“Bioteknolojia si chaguo tena bali ni hitaji la lazima kama tunataka Tanzania iwe na usalama wa chakula, ajira kwa vijana na uchumi wa kisasa unaotegemea sayansi, teknolojia na ubunifu” Alisema Prof. Msoffe.

Alisema bioteknolojia itasaidia pia sekta ya afya kwa kuzalisha chanjo, tiba za jeni na vipimo vya vinasaba vitakavyotambua magonjwa mapema, pamoja na kudhibiti malaria kupitia teknolojia za kisasa za kudhibiti mbu.

Aliongeza kuwa Serikali pia inaendelea kufanya maboresho ya sera na sheria ili kuhakikisha matumizi ya teknolojia hii yanafanyika kwa usalama bila kuathiri binadamu, wanyama na mazingira.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa BST Prof. Peter Msolla alisema Tanzania haina budi kuwekeza katika utafiti wa bioteknolojia katika mazao muhimu kama mahindi, mpunga, mihogo na migomba ili kukabiliana na changamoto za uzalishaji.

Alisema bila utafiti, nchi haiwezi kupata faida kamili za teknolojia hiyo wala kuwajibu wadau wanaohoji usalama wake.

“Bila kuwekeza katika utafiti wa bioteknolojia, Tanzania itaendelea kulima kwa mazoea badala ya kutumia sayansi na hilo litatuacha nyuma katika ushindani wa chakula, biashara na maendeleo.”Alisisitiza Prof. Msolla.

BST pia imekuwa ikielimisha umma kuhusu bioteknolojia ili kuondoa hofu na dhana potofu, huku ikisisitiza kuwa teknolojia hii inaweza kubadili kabisa kilimo na uchumi wa nchi iwapo itaungwa mkono kwa sera rafiki, uwekezaji na uelewa wa jamii.

HABARI PICHA WAKATI WA MKUTANO HUO.

 





Post a Comment

0 Comments