Na: Adam Maruma
Wanawake
wametakiwa kutumia kikamilifu fursa za masomo na mafunzo zinazotolewa na Chuo
Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ili kujijengea uwezo, kuongeza ujuzi na
kuimarisha ushiriki wao katika maendeleo ya jamii.
Wito huo umetolewa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa Mipango, Fedha na Utawala, Prof. Amandus Muhairwa, wakati wa hafla ya kuwapongeza wanawake wa chuo hicho katika maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani yaliyofanyika kwenye ukumbi wa SUA uliopo Nanenane mjini Morogoro.
Prof. Muhairwa amesema kuwa SUA ina mfumo thabiti wa kulinda wanawake na wasichana
pamoja na kutekeleza mpango mkakati wa usawa wa kijinsia, hali inayochangia
kuwepo kwa mazingira salama na yenye utulivu yanayowezesha wanawake kufikia
malengo yao ya kitaaluma na kiutendaji.
Kwa upande wake, Mwakilishi wa Makamu Mkuu wa Chuo ambaye pia ni Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu, Prof. Maulid Mwatawala, amesema kuwa katika uongozi wa Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Raphael Chibunda, wanawake wameendelea kupata nafasi zaidi za uongozi chuoni huku wanafunzi wa kike wakionesha kufanya vizuri kitaaluma.
Prof. Mwatawala amesema kwa sasa chuo kimefikia asilimia 43 katika kuelekea lengo la
usawa wa kijinsia wa asilimia 50 kwa 50. Aidha, amewapongeza wanawake kwa
juhudi zao katika kazi na mchango wao katika maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Ameongeza kuwa chuo kina utaratibu mzuri wa kushughulikia masuala ya unyanyasaji wa kijinsia na kuwahimiza wanawake kutumia kikamilifu fursa za masomo ili kujiendeleza zaidi kitaaluma.
Kwa
upande wao, Mwenyekiti wa RAAWU tawi la SUA, Bw. Faraja Kamendu, na Mwenyekiti
wa THTU tawi la SUA, Bw. Nickson Mkilamwene, wamesema kuwa kuwapa wanawake
nafasi katika ajira na uongozi kunachochea ufanisi wa utendaji kazi katika
taasisi mbalimbali. Viongozi hao pia wamewahamasisha wanawake kufanya kazi kwa
bidii kwa maendeleo ya chuo na kujiunga na vyama vya wafanyakazi ili kulinda
maslahi yao ya kikazi na kitaaluma.
Akisoma
hotuba kwa niaba ya wanawake wa chuo hicho, Bi. Farida Mkongwe ameishukuru
menejimenti ya chuo kwa kuendelea kutoa fursa za mafunzo kwa wanawake, akisema
hatua hiyo imechangia kwa kiasi kikubwa kuongeza ujuzi, uwezo na weledi katika
utekelezaji wa majukumu yao ya kazi.
Ameongeza
kuwa utoaji wa mafunzo kwa watumishi unazingatia mipango na bajeti ya chuo,
huku akiiomba menejimenti kuendelea kupanua wigo wa fursa hizo ili kuwajengea
wanawake uwezo zaidi katika nyanja mbalimbali za kitaaluma na kiutendaji.








0 Comments