SUAMEDIA

RC Malima: Wanawake ni nguzo muhimu ya maendeleo Morogoro.

 Na: Adam Maruma – Morogoro.

Mkuu wa koa wa Morogoro Mhe.Adam Malima amesema wanawake wana mchango mkubwa na wa moja kwa moja katika maendeleo ya mkoa na taifa kwa ujumla ndio maana Tanzania imekuwa mfano barani Afrika katika kuhimiza ushiriki wa wanawake katika shughuli za maendeleo na uongozi.

Mkuu wa Mkoa wa Morogoro Mhe. Adam Malima akizungumza kwenye siku ya wanawake kimkoa Mkoani Morogoro.


Mhe. Malima ameyasema hayo wakiatai akitoa hobutba yake kwenye maadhimisho ya Siku ya Wanawake Duniani iliyofanyika kimkoa katika Tarafa ya Mikese, Kata ya Mikese, Kijiji cha Fulwe mkoani Morogoro.

Aidha alikumbusha kuwa katika historia kulikuwa na nyakati ambapo maadhimisho ya Siku ya Wanawake hayakuweza kufanyika katika baadhi ya maeneo ya Mkoa wa Morogoro na nchini kwa ujumla japo kuwa mapambano ya haki za wanawake yamekuwepo kwa muda mrefu duniani.

Alitoa mfano wa nchi zilizoendelea kama Marekani, ambapo wanawake hawakuruhusiwa kupiga kura hadi mwaka 1920, na kuongeza kuwa kabla ya hapo kulikuwa na changamoto za ubaguzi wa rangi na ajira, na wanawake walikuwa wakilipwa mishahara midogo ikilinganishwa na wanaume.

Aidha, Mkuu huyo wa Mkoa alisema hatua ya wanawake kushika nafasi mbalimbali za uongozi nchini ni mafanikio makubwa kwa taifa, na kukumbusha kuwa mwanamke wa kwanza kuwa Mkuu wa Mkoa wa Morogoro alikuwa Anna Abdallah katika miaka ya 1970.

Hata hivyo, Malima alisema bado kuna changamoto ya unyanyasaji wa kijinsia katika jamii, ikiwemo visa vya wanafunzi wa kike kupata ujauzito wakiwa shuleni na hivyo kutumia nafasi hiyo kuwataka maafisa Maendeleo ya jamii katika Mkoa wa Morogoro, pamoja na Mahakama na madawati ya jinsia, kutokuwa na huruma katika kushughulikia kesi za aina hiyo pindi zinapowasilishwa mbele yao.

Pia alitoa onyo kwa wazazi wanaomaliza kesi za ukatili wa kijinsia kimya kimya majumbani bila kuripoti katika vyombo vya sharia kwani vitendo hivyo vinachangia kuendeleza tatizo hilo na kukatiza ndoto za mabinti wengi na hivyo kuwahakikishia kuwa hatakuwa na huruma kwa kiongozi yeyote katika Mkoa wa Morogoro atakayeshindwa kushughulikia kesi hizo kwa mujibu wa sheria.

Malima aliwataka viongozi kuelewa na kuzingatia Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2050 ili kusaidia kufikia malengo ya maendeleo ya taifa na kuwa nchi zinazokandamiza haki za wanawake haziwezi kupiga hatua za maendeleo.

Maadhimisho hayo hufanyika kila tarehe 8 March ulimwenguni kote, na kwa mwaka huu  katika mkoa wa Morogoro yamehudhuriwa na viongozi wa serikali, wadau wa maendeleo na wananchi, yakilenga kuendelea kuhamasisha usawa wa kijinsia na kutambua mchango wa wanawake katika maendeleo ya jamii.


MATUKIO KATIKA PICHA  SIKU YA WANAWAKE MOROGORO.

 








Post a Comment

0 Comments