Na: Ngolo Mboje
Makamu Mkuu
wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Prof. Raphael Chibunda, amesema kuwa studio mpya za chuo hicho ni nyenzo muhimu
katika uzalishaji wa vipindi vya redio, televisheni na maudhui ya mitandao ya
kijamii vinavyoweza kusaidia kuonesha mchango wa chuo katika maendeleo ya sekta
za kilimo, mifugo, misitu na sayansi.
Prof. Chibunda ameyasema hayo wakati akizungumza na wafanyakazi wa Kitengo cha Mawasiliano na Masomo baada ya kutembelea studio za SUA Media zilizopo chini ya kitengo hicho katika Kampasi ya Edward Moringe, mkoani Morogoro.
Amesema Serikali kupitia Mradi wa Elimu ya Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi
(HEET) imetoa msaada wa kuboresha studio hizo kwa lengo la kuimarisha
uzalishaji wa vipindi vinavyolenga sekta ya kilimo pamoja na kuitangaza SUA kwa
jamii.
Aidha, Profesa Chibunda ametoa wito kwa wanahabari wa SUA Media na watumishi wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko kujipanga vizuri katika uzalishaji wa vipindi mbalimbali, kukifahamu chuo kwa undani pamoja na kuhakikisha wanatunza vifaa vya studio ili viweze kutumika kwa ufanisi na kwa muda mrefu.
Kwa upande wake, Kaimu Mkuu wa Kitengo
cha Mawasiliano na Masoko cha SUA, Bi.
Suzana Mgobeko, ameishukuru Menejimenti ya chuo kupitia mradi wa HEET
kwa kuboresha studio hizo na kuahidi kuwa kitengo hicho kitaendelea kuzalisha
vipindi bora vya redio, televisheni na mitandao ya kijamii vitakavyochangia
kuitangaza SUA na kuimarisha maendeleo ya sekta ya kilimo.


0 Comments