Na: Josephine Mallango
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe, Bi. Shamim Mwariko, amewataka vijana
wa Mpimbwe kutumia Mradi wa TAGDev 2.0
AGRIFOSE–RIH unaotekelezwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kuongeza uzalishaji ili kupata fursa
za masoko ndani na nje ya Tanzania.
“Mradi huu wa TAGDev 2.0 AGRIFOSE–RIH ni mradi wa kipaumbele kwa Mpimbwe, watendaji wote wa Mpimbwe wahakikishe vijana wanawezeshwa ili kupata matokeo mazuri ya mradi huu ambayo ni fursa ya kuonekana na kupata miradi mingine zaidi, wananchi waendelee kunufaika, tuna skimu nne za umwagiliaji, hii ni nafasi yetu tushirikiane na wataalam wa SUA sasa tulete mabadiliko ya kiuchumi Mpimbwe,” amesema Mwariko.
Akizungumza wakati wa kutambulishwa kwa mradi huo mpya
unaotekelezwa chini ya RUFORUM kwa ufadhili wa Mastercard Foundation,
Mkurugenzi huyo amesema nchi nzima ina halmashauri 184 lakini halmashauri nne
pekee ndizo zilizochaguliwa kushiriki katika mradi huo, moja wapo ikiwa
Mpimbwe.
Amesisitiza kuwa vijana wa Mpimbwe wanapaswa kutumia mradi
huu kama chachu ya kufanikisha ndoto zao kwa kuwa unatoa fursa ya kujiajiri na kuajiri
wengine kupitia mnyororo wa thamani wa mazao ya mpunga na bustani, sambamba na
matumizi ya teknolojia bunifu za kilimo na usindikaji.
“Vijana ndiyo waendeshaji wa mageuzi ya kiuchumi duniani
kote,moja ya vitu ambavyo Afrika inaweza kuuza ndani na nje ya nchi ni mazao ya
kilimo, na vijana wa Mpimbwe hawasukumwi kufanya kazi , wanaijua thamani ya
pesa ya kilimo, hivyo, mradi huu utapata matokeo mazuri kwa kuwa umejikita
kuwawezesha vijana katika kilimo cha tija na mnyororo wa thamani, ambapo
hawatatakiwa kutumia nguvu kubwa tena kulima kiholela, bali watatumia
teknolojia, ubunifu na kupata masoko ya uhakika kuanzia maandalizi ya mashamba
hadi uvunaji na masokoni,” amesisitiza Mwariko.
Mkurugenzi huyo ameongeza kuwa wanatarajia matokeo ya mradi
huo yatasaidia kuongeza mapato ya halmashauri na kuinua hali ya kiuchumi ya
vijana kupitia vikundi vyao, amesema vijana zaidi ya 200 kutoka kata saba za Kibaoni, Ikuba, Chamalendi, Mbede, Mwamapuli,
Mamba na Kasansa watanufaika kupitia mafunzo na uwezeshaji wa mradi huo
katika Halmashauri ya Wilaya ya Mpimbwe mkoani Katavi.
Kwa upande wake, Mratibu wa Mradi, Dkt. Hamisi Tindwa, amesema lengo la mradi ni kuwawezesha vijana kupata ujuzi kupitia mafunzo ya vitendo, kuwapatia mitaji ya kuanzia (mbegu), kuunda ajira za kujiajiri na kuajiri wengine, kuongeza uzalishaji na kuwafikisha kwenye masoko ya uhakika.
Ameongeza kuwa vijana 1,000 wenye umri wa miaka 18 hadi 35
pamoja na wakulima zaidi ya 25,000 watanufaika kupitia mafunzo ya mbinu bora za
kilimo na njia za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi.
Wakati wa mafunzo kwa vikundi, Naomi James kutoka kikundi cha Upendo Wanawake Iziwasungu kata ya Kasansa, aliomba mradi
uwasaidie kwa kuwapatia wataalamu wa elimu sahihi ya kilimo cha mpunga, mbegu
bora, matumizi ya viuatilifu na mbolea, pamoja na uwezeshaji wa mitaji na
mashine za kuvunia na kuchakata mpunga ili waweze kupata masoko kwa wingi na
mazao bora zaidi.
Mradi wa TAGDev 2.0
AGRIFOSE–RIH ni sehemu ya Programu ya RUFORUM inayotekelezwa kwa
ushirikiano kati ya Chuo Kikuu cha
Sokoine cha Kilimo (SUA), Chuo
cha Nelson Mandela (Arusha), Chuo
Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM) na Jukwaa la Vyuo Vikuu Afrika (RUFORUM) kwa ufadhili wa Mastercard Foundation. Ni mradi wa
miaka mitano wenye thamani ya Shilingi bilioni 1.6, unaotekelezwa katika
halmashauri nne nchini: Morogoro
Vijijini, Ifakara Mjini, Manispaa ya Morogoro na Mpimbwe Wilaya ya Mlele,
mkoani Katavi.




0 Comments