SUAMEDIA

Elimu ya SUA yazalisha wabunifu wa suluhisho za kidigitali kwa sekta ya mifugo

 Na: Farida Mkongwe

Kampuni ya Afya ya Mnyama Digital Limited, imekipongeza Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa mchango wake mkubwa  katika kuwajengea vijana ujuzi na uwezo wa ubunifu unaochochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Akizungumza katika mkutano wa mwaka wa SUA CEO Alumni Forum 2025, Mwanzilishi Mwenza na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo, Juliet Tarimo, amesema elimu aliyoipata SUA imekuwa chachu muhimu katika mafanikio yake binafsi na ya kampuni yake.

Amesema amefurahia kuona jinsi SUA ilivyowakutanisha wahitimu wa miaka mbalimbali, wakiwemo wakurugenzi na watendaji wanaoendelea kuchangia maendeleo ya taifa kupitia sekta tofauti.

“SUA imenijenga kielimu na kimfumo, kupitia somo la Agriculture Investment and Banking, niliweza kupata maarifa yaliyoniwezesha kuunda kampuni inayotumia teknolojia kusaidia wafugaji,” amesema Juliet.

Kampuni ya Afya ya Mnyama Digital Limited inalenga kuboresha ustawi wa wafugaji kwa kutumia teknolojia ya kidigitali kufuatilia maendeleo ya afya ya mifugo.

Kupitia mfumo huo, wafugaji wanapata taarifa sahihi kuhusu afya za mifugo yao, hatua za matibabu, chanjo na ushauri wa kitaalamu ambao unalenga kuongeza tija katika uzalishaji na kupunguza hasara zinazotokana na magonjwa yasiyotambuliwa mapema, hivyo kuendeleza lengo la taifa la kuongeza uzalishaji wa mifugo wenye ubora na faida.

Aidha Mkurugenzi Mtendaji huyo amewasisitiza wanafunzi wa SUA  kutumia ipasavyo rasilimali zilizopo chuoni, ikiwemo walimu, maabara, na program za mafunzo kwa vitendo, ili kukuza ubunifu unaoweza kuleta mabadiliko makubwa katika jamii.





Post a Comment

0 Comments