SUAMEDIA

SUA na TAWA waokoa mtoto wa Tembo aliyenasa mtegoni Kilombero

Na: Mwandishi wetu

Timu ya wataalamu kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ikiongozwa na Dkt. Richard Samson imefanikiwa kuokoa mtoto wa tembo aliyenaswa na mtego kando ya Mto Ruhidgi, katika Pori la Akiba la Kilombero, Wilaya ya Malinyi mkoani Morogoro.

Moja kati ya Maafisa kutoka TAWA na Madaktari kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo wakimsaidia Tembo huyo mdogo.

Mtoto huyo wa tembo alikuwa amenasa kwa siku mbili kwenye mtego uliotengenezwa kwa kamba ngumu na kujeruhiwa mguu wa mbele, hali iliyokuwa ikihatarisha maisha yake kwa kuwa hakuweza kutembea, kutafuta chakula wala maji.

Uokoaji huo, uliofanyika tarehe 19 Septemba 2025, ulishirikisha wataalamu wa SUA na Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania (TAWA), ambayo inasimamia Pori la Akiba la Kilombero. Baada ya kamba kuondolewa na jeraha kushughulikiwa, mtoto wa tembo alirudi katika afya njema na kuungana na familia yake ya asili, huku akiendelea kufuatiliwa kwa karibu na maafisa wa uhifadhi.

Kwa mujibu wa Sheria ya Uhifadhi wa Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009 na Sera ya Taifa ya Wanyamapori ya 2007, kitendo hicho ni mfano wa utekelezaji wa kivitendo wa vita dhidi ya ujangili na umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali, taasisi za elimu na jamii katika kulinda rasilimali za wanyamapori.

“Uokoaji huu ni mfano halisi wa jinsi elimu, ujuzi wa kitaaluma na ushirikiano kati ya taasisi za Serikali na elimu ya juu unavyoweza kuokoa maisha ya wanyamapori na kudumisha maliasili yetu”, amesema Dkt. Samson.

Kwa upande wake, TAWA imeahidi kuendelea kumlinda mtoto wa tembo huyo hadi atakapoimarika kabisa akiwa na familia yake.

Tukio hili pia linaendana na mkataba wa kimataifa wa CITES (1973) unaolinda wanyamapori walioko hatarini, na linachangia utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs) hususan SDG 15 kuhusu kulinda mifumo ya ikolojia ya nchi kavu, SDG 13 kuhusu kupambana na mabadiliko ya tabianchi, na SDG 17 kuhusu kuimarisha ushirikiano ili kufikia malengo.

Post a Comment

0 Comments