SUAMEDIA

SUA yaja na Mradi wenye lengo la kutoa ajira katika sekta ya kilimo.

 

Na; Siwema Malibiche:

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za elimu ya juu nchini, kimezindua rasmi mradi wa miaka mitano wenye lengo la kuongeza mnyororo wa thamani wa mazao ya mpunga na bustani, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuwawezesha vijana na wanawake kupata ajira bora na stadi za kujiajiri katika sekta ya kilimo.

Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Mipango, Utawala na Fedha Prof. Amandus Muhairwa akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa Mradi wa pili (kulia) ni  Mratibu Mkuu wa Mradi, Dkt. Hamisi Tindwa

Mradi huu unatekelezwa chini ya ufadhili wa shirika la kimataifa lisilo la kiserikali la’Mastercard Foundation’ kupitia jukwaa la vyuo vikuu vya kikanda (RUFORUM), na utatekelezwa kuanzia mwaka 2025 hadi Desemba 2029.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa mradi huo, Mratibu Mkuu wa Mradi, Dkt. Hamisi Tindwa, amebainisha kuwa lengo kuu ni kuwawezesha vijana kupata ujuzi kupitia mafunzo ya vitendo na nadharia katika kilimo cha kisasa, ili kuunda ajira, kuongeza uzalishaji na kufikia soko lenye tija.

 “Kupitia mradi huu, zaidi vijana 1,000 wenye umri kati ya miaka 18 hadi 35 wanatarajiwa kunufaika kwa kupata ajira bora. Vilevile, wakulima zaidi ya 25,000 katika maeneo ya utekelezaji wa mradi watafikiwa na kupewa mafunzo juu ya mbinu bora za kilimo pamoja na njia za kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi,” amesema Dkt. Tindwa.

Mradi huu pia unalenga kuwajengea vijana uwezo wa kuajirika na kujiajiri katika sekta ya kilimo, hasa katika mnyororo wa thamani wa mazao ya mpunga na bustani, huku ukitilia mkazo matumizi ya teknolojia bunifu za kilimo na usindikaji.

Aidha, Rasi wa Ndaki ya Kilimo katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) na Kiongozi Mshiriki wa Mradi, Dkt. Nyambilila Amuri,    ameeleza kuwa mradi huu ni fursa adhimu kwa vijana kushiriki kikamilifu katika kupanua mnyororo wa thamani katika sekta ya kilimo kwani umelenga kuwashawishi na kuwahamasisha wakulima kujiunga na kuwekeza katika kilimo kwa kuwapatia mazingira rafiki, teknolojia bunifu na stadi muhimu zitakazowasaidia kufanya kilimo chenye tija na chenye mchango mkubwa kwa maendeleo ya taifa

Kwa upande wake, Dkt. Leonard Binamungu, Mhadhiri kutoka Idara ya Sayansi na Uhandisi wa Kompyuta, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, amesisitiza umuhimu wa ushiriki wa vijana katika mradi huo, akieleza kuwa teknolojia ni nyenzo muhimu katika kuboresha kilimo na kuongeza tija.

“Sisi kama wataalamu wa teknolojia tuna mengi ya kuwafundisha vijana. Kupitia mradi huu, vijana wataweza kujifunza namna ya kubuni mifumo ya kidigitali itakayowawezesha wakulima kupata masoko kwa urahisi na kwa ufanisi zaidi,” amesema Dkt. Binamungu.

Mradi huu unatekelezwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa ushirikiano na Chuo Kikuu cha Nelson Mandela Arusha, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, na Taasisi ya Teknolojia Dar es Salaam (DIT). Moja ya mikakati ya utekelezaji ni kuhuisha mitaala ya vyuo ili iendane na mahitaji ya sasa ya soko na kuhimiza ubunifu wa teknolojia mpya za uzalishaji na kuongeza thamani kwenye mazao.










Post a Comment

0 Comments