SUAMEDIA

Wakulima wahimizwa kutumia Ghala la Mkulima SUA kupata maarifa na teknolojia za kisasa

 Na: Siwema Malibiche

Wakulima wametakiwa kutumia Ghala la Mkulima kutoka Maktaba ya Taifa ya Kilimo iliyopo katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupata maarifa, ujuzi na teknolojia mbalimbali za kilimo ili kuongeza tija na faida katika uzalishaji wa mazao.

Wito huo umetolewa na Mkutubi na Msimamizi kutoka Idara ya Rejea na Huduma kwa Jamii wa Maktaba hiyo, Bw. Jabir Jabir, katika maonesho ya wakulima yanayoendelea Kanda ya Mashariki mkoani Morogoro, ambapo amesema kilimo bora ni kile kinachofanyika kwa kufuata taarifa na maarifa sahihi kutoka kwa wataalamu.

Ameeleza kuwa licha ya kuwepo kwa vitabu vingi ambavyo wakulima wanaweza kuvisoma, pia wanaweza kujifunza kwa njia ya mtandao kwa kutumia simu janja kupitia "Mkulima Collection", ambapo hupata mafunzo mbalimbali kutoka kwa wataalamu waliobobea katika sekta ya kilimo.

Amesema maktaba hiyo inakawaribisha watu wa kada zote kupata maarifa bila kujali kiwango cha elimu, na kusisitiza kuwa katika kitengo cha Ghala la Mkulima wanakusanya taarifa na machapisho mbalimbali yanayotokana na tafiti zilizofanywa na SUA pamoja na watafiti wengine kutoka taasisi mbalimbali, yaliyoandikwa kwa lugha rahisi inayomuwezesha mkulima kuelewa kwa urahisi.

Vile vile, ameitaka jamii kujikita zaidi katika kutafuta maarifa ya kilimo kabla ya kuanza shughuli za kilimo ili kufanikisha uzalishaji wenye tija. Amesisitiza kuwa SUA ina machapisho mengi ambayo yanaweza kumsaidia mkulima kujisomea akiwa mahali popote duniani.

Maktaba ya Taifa ya Kilimo iliyopo SUA Kampasi ya Edward Moringe inalenga kusaidia wakulima kupata taarifa muhimu kuhusu kilimo, mifugo na uvuvi ambapo kupitia machapisho mbalimbali, wakulima wanaweza kuboresha ufanisi wa kazi zao kwa kupata maarifa ya kitaalamu yanayozingatia tafiti na teknolojia za kisasa.




Post a Comment

0 Comments