SUAMEDIA

SUA yawahakikishia wanafunzi usalama imara chuoni

 Na: Ayoub Mwigune

Polisi Wasaidizi wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), limewahakikishia wanafunzi wanaotamani kujiunga na Chuo hicho kuwa hali ya usalama ndani ya mazingira ya chuo ni shwari na kuwa ulinzi umeimarishwa kwa kiwango cha hali ya juu ili kuhakikisha mazingira bora ya kujifunzia na kuishi.

Akizungumza katika mahojiano maalum na SUA FM katika viwanja vya maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki yanayofanyika mkoani Morogoro, Msimamizi wa Polisi Wasaidizi SUA ambaye pia ni Msaidizi wa Kamishna wa Polisi (ACP), Simon Haule amesema askari wa SUA wamejidhatiti kuhakikisha kuwa kila mwanafunzi anayekuja SUA anakuwa salama kwa wakati wote akiwa chuoni.

"Tunaendelea kuwajengea uwezo askari wetu kupitia mafunzo na miongozo ya kiusalama, lengo letu ni kuhakikisha kila mwanafunzi anasoma na kuishi katika mazingira ya amani bila hofu yoyote kwani ulinzi hapa SUA si suala la bahati nasibu, ni wajibu wetu wa kila siku," amesema ACP Haule.

Kwa upande wake, Mrakibu wa Polisi Msaidizi (SP) Nicholaus Mwamtobe ambaye ni Msaidizi wa Mkuu wa Idara ya Usalama SUA, amesema kuwa Chuo kimewekeza vya kutosha katika mifumo ya kiusalama ikiwemo doria za mara kwa mara, matumizi ya CCTV pamoja na ushirikiano na vyombo vingine vya usalama.

"Tumeimarisha doria usiku na mchana, ndani na nje ya Chuo, na tumewahimiza wanafunzi kuzingatia miongozo ya kiusalama inayotolewa na uongozi, huu ni mpango shirikishi ambao tunautekeleza kwa weledi mkubwa," amesema SP Mwamtobe.



Post a Comment

0 Comments