SUAMEDIA

SUA yatangaza teknolojia ya ndege nyuki kuongeza tija ya kilimo nchini

 Na: Ayoub Mwigune

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kuwa kinara wa mageuzi katika sekta ya kilimo nchini kwa kutambulisha teknolojia ya kisasa ya ndege nyuki (drones) kwa matumizi ya kilimo, hususan katika usambazaji wa viuatilifu na mbolea mashambani.

Akizungumza katika maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki wakati wa mahojiano maalum na SUA Media, Afisa Kilimo wa SUA, Bi. Fatuma Hassan amesema matumizi ya ndege nyuki ni miongoni mwa mbinu za kisasa zenye uwezo wa kuongeza tija kwa wakulima kwa usahihi na ndani ya muda mfupi.

Amesema teknolojia hiyo ina uwezo wa kupulizia dawa au mbolea katika eneo kubwa bila mkulima kuingia shambani, hivyo kumuepusha na madhara ya moja kwa moja yatokanayo na kemikali.

Bi. Fatuma ameongeza kuwa SUA imeendelea kuwa mstari wa mbele katika kutoa mafunzo ya mbinu bora za kilimo pamoja na matumizi ya teknolojia mbalimbali ambapo kwa sasa, Chuo hicho kimeanza rasmi kutoa mafunzo maalum ya matumizi ya ndege nyuki kwa vijana wanaosomea kozi za kilimo, kwa lengo la kuwajengea uwezo wa kutatua changamoto zinazowakabili wakulima katika jamii na Taifa kwa ujumla.

"Teknolojia hii inalenga kuongeza ufanisi katika shughuli za kilimo kwa kupunguza muda wa kazi, gharama na athari za kiafya kwa wakulima," amesema Bi. Fatuma.

Aidha, amesema matumizi ya teknolojia hiyo yamesaidia kupunguza gharama na muda wa kazi mashambani, kulinda mazingira, na kuimarisha afya ya wakulima kwa kuwaepusha na athari za moja kwa moja za kemikali.




 

Post a Comment

0 Comments