SUAMEDIA

Wahitimu SUA wabuni mfumo wa kidigitali kuboresha afya ya mifugo

 

Na: Josepuhine Mallango

Wahitimu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wamekuja na Mfumo wa Afya ya Mnyama Digital ambao umeelezwa kuwa ni muhimu na rafiki kwa maendeleo ya mashamba ya wafugaji katika kuongeza uzalishaji na kipato sambamba na kusaidia kupunguza gharama za uzalishaji.



Teknolojia ya Afya ya Mnyama Digital ilianzishwa mwaka 2024 na wanafunzi wahitimu kutoka SUA walioungana kama kundi kwa lengo la kutumia ujuzi wao kutoka kozi mbalimbali ikiwemo Taaluma ya Tiba ya Wanyama, Biashara, Masuala ya Kibenki na Teknolojia ambapo kupitia ushirikiano huo, walikuja na wazo la kuwasaidia wafugaji kufuatilia kwa urahisi maendeleo ya afya ya wanyama wao kwa wakati, jambo lililowapelekea kubuni mfumo huo wa kidigitali kama suluhisho la kiteknolojia kwa changamoto hiyo.

Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Afya ya Mnyama Digital, Julieth Tarimo, wakati akizungumza na SUA Media katika Maonesho ya Nanenane, ambapo amesema ni muhimu zaidi kutumia mfumo wa Afya ya Mnyama Digitali ambao ni teknolojia ya kuweka tagi ya kidigitali ya sikio (smart ear tag sensor) kwa sababu ni huduma inayomsaidia mkulima kupata taarifa za maendeleo na kufuatilia kwa ukaribu mnyama wake anapopata changamoto inamsaidia kupata taarifa sahihi na za haraka na na hivyo kujua maendeleo ya mnyama wake.



"Faida ya kutumia mfumo wa mnyama Afya Digital ni kwamba mnyama wako akipata changamoto ni rahisi sana kujua kwa kuwa taarifa zake zinajituma katika mfumo, ambapo ni tofauti na kawaida ambapo ng’ombe akipata changamoto siyo rahisi kujua labda mpaka uone kwa macho, na kwamba walianzisha mfumo huu baada ya kuona wafugaji walio wengi huwa wanachelewa kujua mpaka wamuone mnyama kwa macho, wakati mwingine changamoto inakuwa imefikia hatua ya kutotatulika na kusababisha madhara," amesema Julieth.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Afya ya Mnyama Digitali, Mabula Marko, amesema mfumo wa kidigitali mpaka sasa umeshahudumia zaidi ya ng’ombe 1000 katika mikoa ya Morogoro, Kagera na Shinyanga kwa kuweka tagi ya kidigitali, na kwamba mfumo huo umetengenezwa kwa mazingira ya kitanzania zaidi ambapo unaweza kutumika katika mazingira yote ya vijijini na mjini.

Pia, ukiwa mbali na mifugo yako, unafunga tagi ya sikio na bado una uwezo wa kufuatilia mifugo yako popote unapokuwa, tofauti na hapo awali ambapo ilikuwa lazima uwe karibu na eneo la mifugo.

Mkurugenzi huyo ameongeza kuwa faida ambazo ziko kwenye mfumo wa Afya ya Mnyama Digitali ni pamoja na mfugaji kupata taarifa za madaktari waliosajiliwa na Baraza la Madaktari Tanzania, kupata madawa na kiwango kinachoruhusiwa kutumika katika mashamba ili kuongeza uzalishaji unaotokana na ufugaji.

Amesema gharama za mfumo ni shilingi 50,000/= kwa ng’ombe mmoja kuwekewa tagi ya kidigitali ya sikio, ambapo kutokana na mazingira ya wafugaji wa Kitanzania wameweka mazingira ya kulipia kidogo kidogo mpaka mfugaji anamaliza na kubaki na tagi hiyo moja kwa moja.

Amesema endapo mnyama atakufa, tagi hiyo inaweza kuhamishiwa kwa mnyama mwingine, hivyo amewataka wafugaji kufika kwa wingi katika banda lao la Afya ya Mnyama Digital ili kupata elimu na huduma ya afya ya mnyama kwa njia ya kidigitali.




Post a Comment

0 Comments