Na: Vumilia Kondo
Wataalamu wa mifugo kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA)
wameeleza kuwa kilimo cha malisho bora ya wanyama kinaweza kuwa suluhisho la
kudumu la migogoro inayojitokeza mara kwa mara kati ya wakulima na wafugaji
nchini.
Akizungumza katika maonesho ya kilimo ya Nanenane yanayoendelea mkoani Morogoro, Ahmed Amasha ambaye ni Afisa mifugo kutoka SUA amesema kuwa kupitia teknolojia ya kuzalisha malisho ya kisasa kwenye maeneo madogo, wafugaji wanaweza kupunguza utegemezi wa kutangatanga kutafuta chakula cha mifugo.
Amasha amesema banda la mafunzo
ya mifugo kutoka SUA limeonesha aina tatu kuu za malisho ambayo yanaweza kuleta
tija kwa wafugaji bila kuathiri shughuli za kilimo.
“Tunayo malisho ya jamii ya mikunde kama Alfa Alfa na Russian Confrey ambayo yana protini ya kutosha na huongeza virutubisho kwa mifugo. Pia tunayo
majani tembo kama Local Napia na Giant Juncao ambayo hustahimili ukame na kutoa mazao
ya kutosha,” amesema Amasha.
Aina nyingine ya malisho iliyotajwa ni nyasi za malisho kama Rhodes, Brachiaria, Cencrus ambazo zinaweza kulimwa, kukatwa na kuhifadhiwa kama lishe ya wanyama hasa wakati wa kiangazi.
Kwa mujibu wa Amasha, baadhi ya majani hayo kama Giant Juncao yana uwezo wa
kutoa mavuno hadi tani 180 kwa mwaka kwenye hekta moja na yana protini ya hadi
asilimia 18, hivyo kusaidia kukuza mifugo ya maziwa na nyama kwa haraka.
“Kwa kutumia malisho haya, mfugaji anaweza kulisha mifugo bila kutoka
nje ya shamba lake. Hii inaondoa migogoro na wakulima kwa sababu hakuna
kutangatanga. Pia, malisho haya yanaweza kulimwa kibiashara na kuuza kwa
wafugaji wengine,” ameongeza.
Aidha, ametoa wito kwa wafugaji kuanza kuwekeza kwenye kilimo cha malisho badala ya kuongeza idadi ya mifugo pasipo kuwa na uhakika wa lishe.
“Tunahamasisha wafugaji kulima majani haya ili wawe na mifugo michache
yenye tija kuliko kuwa na makundi makubwa yasiyo na faida,” amesema.
Maonesho ya Nanenane yameendelea kuwa jukwaa la kuonesha teknolojia
mbalimbali za kilimo na mifugo huku SUA ikijitokeza kuhamasisha matumizi ya
mbinu za kisasa katika ufugaji na uzalishaji wa chakula cha mifugo.







0 Comments