SUAMEDIA

SUA yatumia makambi ya mafunzo kuandaa wataalamu wa utalii wa vitendo

 Na: Vumilia Kondo

 Katika juhudi za kuhakikisha elimu ya utalii haiishii darasani, Idara ya Utalii na Mapumziko huishi  ya Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine (SUA) imeendelea kuandaa makambi ya mafunzo (camping) kwa wanafunzi wake kama sehemu muhimu ya mafunzo ya vitendo.


 Simmy Thadeo, Mkufunzi katika idara hiyo amesema camping ni zaidi ya safari ya kawaida , ni jukwaa la kujifunza, kujitambua, na kujiandaa kitaaluma katika mazingira halisi ya kazi.

 “Camping ni sehemu ya mtaala wetu wa mafunzo, tunawapeleka wanafunzi porini au kwenye maeneo ya vivutio vya utalii ili wajifunze kwa vitendo kila kitu walichofundishwa darasani kuanzia upangaji wa safari, huduma kwa wageni, hadi masuala ya mazingira na usalama,” anasema Thadeo.

 Makambi hayo huandaliwa kwa muktadha wa mafunzo ya fani mbalimbali ndani ya utalii, ambapo wanafunzi hupangwa katika timu na kupewa majukumu kama walivyo wahudumu au waongoza watalii kwenye maeneo ya hifadhi au vivutio vya asili.

“Kama hutaweza kupanga ratiba ya wageni, kupokea mgeni, au kujua namna ya kuwahudumia vizuri , hujawa mtaalamu wa utalii, Camping inajenga stadi hizi moja kwa moja,” amesisitiza.

 Mbali na stadi za kitaaluma, wanafunzi hujifunza uongozi, kazi kwa pamoja, na kutumia rasilimali chache kwa ufanisi, hii huwasaidia kujiandaa kukabiliana na changamoto katika mazingira halisi ya kazi.

“Wanafunzi huandaa ratiba, hupika, hulala kwenye mahema, na kushughulika na mazingira halisi ya kazi, ni uzoefu ambao hubadilisha namna wanavyoelewa taaluma yao,” amesema Thadeo.

Kwa sasa, Idara inaendelea kuimarisha ushirikiano na wadau wa sekta ya utalii na mazingira, huku ikiandaa wanafunzi wanaoweza kushindana katika soko la ajira kwa ujasiri na weledi.

“Tunawaandaa kuwa si tu waajiriwa bora, bali pia wabunifu na watoa suluhisho katika sekta ya utalii na mapumziko,” ameeleza  Thadeo.

 


Post a Comment

0 Comments