SUAMEDIA

SUA yateuliwa rasmi kuwa Makao Makuu ya CEBOT Afrika

 Na: Hadija Zahoro

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimetangazwa kuwa Makao Makuu ya Jukwaa la Kimataifa linalolenga kuimarisha ubadilishanaji wa maarifa, teknolojia na biashara katika sekta ya kilimo na biashara Afrika (CEBOT), kutokana na mchango wake mkubwa katika tafiti za kilimo, ubunifu wa teknolojia, na maendeleo ya mifumo endelevu ya uzalishaji wa chakula.

Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati mpana wa kukuza ushirikiano wa kimataifa katika maendeleo ya kilimo na biashara kwa kutumia rasilimali na tafiti zinazofanyika barani Afrika, hususan kupitia taasisi zinazotambulika kitaaluma kama SUA.

Akizungumza katika hafla maalum ya uzinduzi iliyofanyika SUA ikihusisha Menejiment ya Chuo hicho, Mkurugenzi wa Taasisi ya CEBOT na wawakilishi wake, Mkurugenzi Msaidizi wa Masuala ya Utawala na Maendeleo ya Biashara Barani Afrika, Denice Christian, ameeleza kuwa uteuzi wa SUA umetokana na ukubwa wa Chuo hicho kitaaluma, pamoja na mchango wake katika masuala mtambuka ya kilimo, mazingira, ujasiriamali na ubunifu mbalimbali.

“Wapo vijana wanaomaliza masomo yao lakini hawapati ajira, hivyo tukaona tuanzishe kituo cha ubunifu ambapo makao makuu yatakuwa SUA  kwa ukanda wa Afrika, na DIT kwa masuala ya teknolojia, huku SUA ikisimamia upande wa kilimo, makao makuu yetu yapo Marekani,” amesema Denice.

‘‘Kama mnavyojua kwa sasa  hakuna misaada (USAID),sasa hivi tunaingia kwenye utawala wa kibiashara ndiyo maana tukasema kwamba tuanzishe ofisi SUA kwani ni Chuo ambacho kina wanafunzi wengi na kitaweza kuunganisha vyuo vyote vya kilimo ukanda wa Afrika’’ ameongeza Denice.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Shahada za Uzamili, Utafiti, Uhaulishaji wa Teknolojia na Ushauri wa Kitaalam SUA, Prof. Japhet Kashaigili, ameeleza kuwa hatua hiyo inawapa fursa ya kutekeleza makubaliano ya ushirikiano kwa kushirikiana katika teknolojia mbalimbali zinazohusu mnyororo mzima wa thamani wa kilimo, ikiwemo uzalishaji wa mazao shambani pamoja na mifugo.

Kwa sasa SUA tayari imeanzisha miradi kadhaa inayolenga kuongeza tija ya kilimo kupitia matumizi ya teknolojia na ubunifu, hatua inayotajwa kuwa msingi wa mafanikio ya CEBOT katika kipindi cha miaka mitano ya ushirikiano huo (2025–2030).




Post a Comment

0 Comments