SUAMEDIA

Wakulima waiomba Serikali kuanzisha kituo cha masoko kwa mazao ya kilimo cha ikolojia

 Na: Josephine Mallango

Serikali imeombwa kuanzisha kituo maalum cha bidhaa zinazotokana na kilimo cha ikolojia ili kumuwezesha mkulima kupata soko la uhakika.


Hayo yamesemwa na wakulima kutoka maeneo mbalimbali walioko katika maonesho ya Nanenane ndani ya mabanda ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), hususan katika banda la Kitovu cha Kilimo Ikolojia, ambapo wamesema wamekuwa wakitekeleza kilimo kinacholinda mazingira kwa kutumia njia za asili, ikiwemo matumizi ya mimea tiba kwa kutibu mimea mingine.

Mkulima Juma Koba kutoka Mgambazi, kata ya Magandu, wilaya ya Morogoro amesema wakulima wa kilimo cha ikolojia wanakabiliwa na changamoto ya bei sokoni, ambapo bidhaa zao huuzwa kwa bei sawa na bidhaa za kilimo cha kawaida, licha ya kuwa kilimo cha ikolojia kinachukua muda mwingi na huzalisha mazao machache.

Naye Daudi Tesha, mkulima kutoka wilaya ya Mvomero, amesema changamoto nyingine ni kwa walaji wanapofika sokoni, mara nyingi huangalia mazao kwa muonekano wa nje tu, na mara nyingine hayawavutii kwa sababu ya rangi au ukubwa, hali inayowafanya kupuuza bidhaa za kilimo cha ikolojia.

Kwa upande wake, mkulima Linah Wilson kutoka Gairo amesema kuwa Serikali inapaswa kuwaangalia kwa karibu zaidi wakulima wa kilimo cha ikolojia kwa sababu ni wachache na wanalima kwa njia salama inayotunza mazingira.

Ameongeza kuwa kuanzishwa kwa kituo maalum cha masoko kwa mazao ya kilimo cha ikolojia kutawanufaisha wakulima kwa kupata soko la uhakika, bei nzuri, na kuongeza hamasa kwa wengine kulima kwa kutumia mbinu zisizotegemea kemikali za viwandani.



Post a Comment

0 Comments