Na: Josephine Mallango
Maonesho ya Nane Nane Kanda ya
Mashariki, Morogoro, yana bahati ya kuwa na Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo
(SUA), Chuo muhimu nchini kilichosheheni maprofesa na wataalam wengine wa
kutosha wa kilimo na kwamba kilichobaki ni kwa viongozi wa Kanda ya Mashariki
kutoka mikoa ya Tanga, Dar es Salaam, Pwani na Morogoro kushirikiana na SUA ili kuongeza tija katika
kilimo.
"Nimetembelea banda la SUA, nimekuta kuna watoto wa shule ndiyo wanalima mboga mboga, Nimejionea teknolojia za hali ya juu na wale watoto wamepata hamasa ya kuahidiwa na Mkoa kupewa motisha ya shilingi laki moja kila mmoja akilima bustani ya kisasa nyumbani, nimejionea teknolojia wanazotumia, zinaleta tija katika kilimo.”
“ Maonesho haya ya Morogoro
yana bahati ya kuwa na SUA ndani ya maonesho, Chuo muhimu kwa maendeleo ya
kilimo, shirikianeni ili teknolojia na ujuzi huo uwafikie wananchi wa vijijini
wa Tanga, Dar es Salaam, Pwani na Morogoro, walime kilimo cha tija, ni kilimo
chenye manufaa," amesema Mhe. Pinda.
Hayo
yamesemwa na Waziri Mkuu Mstaafu, Mhe. Mizengo Pinda, ambaye kwa sasa ni Mshauri
wa Rais katika masuala ya kilimo, wakati wa ufunguzi wa Maonesho ya Nanenane
Kanda ya Mashariki yanayofanyika katika Viwanja vya Mwl. Julius Nyerere mjini
Morogoro, Agosti 2, 2025.
Mhe. Pinda amesema viongozi hao wa mikoa minne kutoka Tanga, Dar es Salaam, Pwani na Morogoro wasilale, waungane kutafuta suluhisho la kudumu ili kusonga mbele katika sekta ya kilimo, uvuvi, ufugaji na misitu, kutokana na kuwa sehemu kubwa ya wananchi wamejiajiri katika sekta hizo kwa zaidi ya asilimia 65 hadi 70.
Ameongeza
kuwa sasa kilimo kinahitaji kutumia dhana za kisasa ambazo zitaendelea kuongeza
tija, kufuatia matumizi ya mbolea na mbegu bora nakwamba matumizi ya dhana za
kisasa yatasaidia zaidi kuongeza tija huku akikemea kilimo cha jembe la mkono,
akisema siyo rafiki kwa mazingira yaliyopo kwani kinafanya kilimo kuonekana
kuwa ni kazi ngumu.
Waziri
Mkuu huyo Mstaafu amewataka viongozi wa Kanda ya Mashariki kuangalia fursa
zilizolala ili waweze kuziamsha kwa ajili ya maendeleo ya nchi, kutokana na
kuwepo kwa mapori mengi yanayonawiri.
Amesema kama mapori hayo hayawezi
kutumika kwa kilimo, basi yatumike kwa ajili ya hewa ukaa, aidha, amesisitiza
kuwa Maonesho ya Nanenane yasiwe jambo la mazoea tu kwamba yakifika tarehe
yanafanyika, bali yatumike kuleta mawazo mapya ya kuboresha na kushauri ambapo
ametoa pendekezo kuwa kila mwaka kifanyike kikao cha maandalizi kabla ya
maonesho ili kuangalia yaliyofanyika, na tathmini ifanyike kila baada ya miaka
mitano.
Kwa
upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Mhe. Adam Malima amesema Maonesho ya
Kanda ya Mashariki ndiyo bora zaidi nchini, na kwamba wanatarajia mahudhurio ya
watu kuwa makubwa zaidi ukilinganisha na mwaka jana, kutokana na maandalizi
yaliyofanyika kwa ufanisi mkubwa.
Ameongeza kuwa kwa mara ya
kwanza katika maonesho hayo kutakuwa na banda la Mkoa litakalotoa mafunzo ya
kilimo, uvuvi na misitu, ambapo kutakuwa na wataalam wa kutosha.
Mhe.
Malima amesema lengo la maonesho hayo ni kujenga ukaribu zaidi na kuvutia watu
mbalimbali, hususan wananchi wa mikoa ya Kanda ya Mashariki na mikoa mingine,
kuja kujifunza kwa tija ili kuondokana na ile sura kuwa kilimo ni jambo gumu.
Kaulimbiu ya mwaka huu katika
Maonesho ya Nanenane ni: Chagua Viongozi Bora kwa Maendeleo ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi 2025.
0 Comments