SUAMEDIA

Panya wanaoshindwa mafunzo huwekwa kwenye makazi ya wazee na wastaafu : SUA

 Na: Josephine Mallango

Mkufunzi na Msimamizi wa Mafunzo ya awali kwa panya kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Priscus Mramba, amesema kuwa panya wanaoshindwa kufuzu mafunzo yao, ambayo huchukua kati ya miezi 8 hadi 9, hubadilishiwa aina ya mafunzo, na endapo watashindwa kabisa, huwekwa katika eneo maalum la panya wazee na wastaafu, ambako huishi hadi kufa kwao.

Akizungumza na SUA Media katika mabanda ya Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA), Mkufunzi huyo amesema kuwa pamoja na mafanikio yanayoendelea kupatikana kupitia panya hao ambao hutumika kugundua mabomu katika nchi mbalimbali kama Kambodia, Azerbaijan, Angola, Ethiopia na Msumbiji, hapa nchini panya hao hutumika kwenye viwanja vya ndege kugundua nyara za Serikali.

Amesema wakati wa mafunzo, baadhi ya panya hukumbwa na changamoto kama kuugua, ambapo hupatiwa matibabu, na kwa wale wanaoshindwa kabisa kufuzu huchukuliwa kwa utaratibu maalum, huwekwa kwenye mapumziko, hupewa mafunzo mbadala, na hupimwa kwa majaribio mbalimbali ili kubaini uwezo wao wa kutambua sampuli endapo wameshindwa hatua zote, hupelekwa rasmi kwenye eneo la wastaafu.

Mramba ameongeza kuwa kabla ya panya kupelekwa kwenye eneo la wastaafu, hufundishwa programu nyingine kwa mfano, kama ameshindwa kufuzu kwenye programu ya mabomu, anaweza kuhamishiwa kwenye programu ya utambuzi wa kifua kikuu (TB) au katika kazi za uzalishaji.

Amesisitiza kuwa panya hao hawawezi kurudishwa porini kwani tayari wameingia kwenye kumbukumbu za kimataifa za wanyama waliopitia mafunzo rasmi, hivyo hutunzwa hadi kufa kwao.

Amesema panya wanaotumiwa katika mafunzo ya kugundua mabomu na kifua kikuu ni aina ya panya buku, na kwamba Watanzania wamekuwa wakipewa kipaumbele katika nchi zote ambazo panya hao wamepelekwa. Aidha, baadhi ya Watanzania wamepata ajira katika nchi hizo pale zinapohitaji huduma ya panya waliopitia mafunzo hayo.

Post a Comment

0 Comments