SUAMEDIA

Kupima udongo na mbegu ni hatua ya kuepuka hasara kwa mkulima : SUA

 

Na: Josephine Mallango 

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Idara ya Sayansi ya Udongo na Jiolojia kimesisitiza kuwa ni muhimu kwa mkulima anayelenga kulima kwa tija kuhakikisha anapima afya ya udongo pamoja na afya ya mbegu atakazozitumia kabla ya kuanza shughuli za kilimo, ili kuepuka hasara na kuongeza ufanisi wa uzalishaji.

Dkt. Hellen Kayagha kutoka SUA amesema katika Maonesho ya Nanenane yanayoendelea, Chuo hicho kinatoa huduma ya bure ya upimaji wa afya ya udongo, mimea na mbegu.

Amesema huduma hiyo inatolewa kwa wakulima na wageni mbalimbali wanaotembelea banda la SUA, ambapo sampuli zinapokelewa na majibu hutolewa ndani ya saa moja tu, hapo hapo bandani.

“Kwanini ni muhimu mkulima kupima udongo, kwa sababu inamsaidia kufahamu kiasi cha virutubisho kilichopo katika udongo na inampa uwezo wa kujua aina ya mbolea anayotakiwa kutumia na aina gani ya virutubisho ambavyo vinatakiwa kuongezwa kwenye udongo wake ili aweze kulima kwa tija na kupata mazao bora na yenye afya bora,” amesema Dkt. Kayagha.

Kwa upande wa mbegu, amesema mkulima anapoangalia afya ya mbegu anazotumia atakuwa na uhakika wa mbegu anayopanda inaota kwa kiasi gani shambani.

Ameongeza kuwa SUA wanafundisha njia rahisi za kufanya majaribio ya uotaji wa mbegu kabla ya kupeleka shambani, jambo litakalomsaidia mkulima kuepuka hasara za kupanda na kurudia tena badala yake, atapanda mbegu akiwa na uhakika kuwa ikipandwa itaota shambani.

Dkt. Kayagha amebainisha kuwa pamoja na kwamba wanapatikana Nanenane kwa sasa kwenye mabanda ya maonyesho wakiwa na vifaa vya kisasa ikiwemo maabara ya udongo inayojibika (mobile soil laboratory testing kit) yenye uwezo wa kupima virutubisho vinavyopatikana kwenye udongo ikiwemo tindikali, huduma hizo zinaendelea kupatikana chuoni ambako kuna vifaa vya kisasa na gharama za upimaji ni nafuu kabisa ambazo mkulima yoyote anaweza kumudu.




Post a Comment

0 Comments