Na:
Hadija Zahoro
Kitovu cha Kilimo Ikolojia kimeendelea kuwa
kiunganishi muhimu kwa wadau mbalimbali wa kilimo hicho nchini, wakiwemo
Mashirika, Serikali pamoja na watu binafsi ambao wamekuwa mstari wa mbele
kuwafundisha wakulima mbinu za kilimo ikolojia kwa lengo la kulinda afya za
wazalishaji, watumiaji pamoja na mazingira.
Akizungumza na SUA Media katika banda la Kitovu cha Ikolojia SUA kwenye Maonesho ya 32 ya Nanenane 2025, Mtafiti Msaidizi kutoka Kitovu hicho kilichopo Idara ya Ugani na Maendeleo ya Jamii, Doris Shayo, amesema wakulima walioshiriki katika maonesho ya mwaka huu ni wale waliotolewa na wadau wa kilimo ikolojia ambao hufanya kazi moja kwa moja na wakulima hivyo imekuwa rahisi kwao kuzungumza lugha moja na kufundishana kwa ufanisi.
Mtafiti huyo amesema badala ya watafiti peke
yao kuwaeleza wakulima kuhusu faida za kilimo ikolojia, wanawahimiza wakulima
kutembelea banda la Kilimo Ikolojia ili kujifunza moja kwa moja kutoka kwa
wenzao wanaotekeleza mbinu hizo kwa vitendo katika maeneo yao na kwa lugha
wanayoielewa.
Aidha, amesema kuwa ili kuongeza thamani ya
mazao yatokanayo na kilimo ikolojia, Kitovu cha Kilimo Ikolojia kwa sasa
kinafanya kazi na Shirika la Kilimo Endelevu Tanzania (Sustainable Agriculture in Tanzania SAT) ambalo hununua mazao hayo moja kwa moja kutoka kwa wakulima na kuyauza
kwa bei nzuri ndani na nje ya nchi.
“Kwa sasa tunafanya kazi na SAT (Sustainable
Agriculture in Tanzania) ambao wamechukua hatua ya kwenda kwa wakulima na
kununua mazao moja kwa moja kutoka kwao, lakini pia wameweza kutengeneza
vikundi vya wakulima ambavyo vina sauti moja ya kuuza kwa bei nzuri zaidi,”
amesema Doris.
Kwa upande wake, Juma Koba, mkulima mdogo kutoka Kikundi cha Faraja Mgambazi kilichopo SUA mkoani Morogoro, amesema kilimo ikolojia ni rafiki kwa mazingira kwani hakitumii kemikali yoyote katika uzalishaji wake, bali hutegemea mboji na samadi zinazotokana na mabaki ya mimea.
Ameongeza kuwa wakulima wa kilimo ikolojia
hutumia mimea dawa kama mipapai
na pilipili kichaa, ambapo
hupondwa, kuchanganywa na maji na kisha kupulizwa kwenye mimea ili kusaidia
kuzuia wadudu na magonjwa, na hivyo kutoa mazao bora na salama kwa matumizi ya
binadamu.


0 Comments