SUAMEDIA

DC Bagamoyo aipongeza SUA kwa kutatua changamoto za malisho ya mifugo

 Na: Hadija Zahoro

Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo, Mhe. Shaibu Ndemanga, amepokingeza Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kwa mchango wake mkubwa katika kusaidia wakulima na wafugaji nchini kupitia tafiti za kisayansi zinazolenga uzalishaji wa malisho bora kwa mifugo.

Akizungumza na SUA Media wakati akitembelea banda la SUA katika maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki mkoani Morogoro, Mhe. Ndemanga  amesema SUA imekuwa msaada mkubwa kwa jamii, hususan kwa wakulima na wafugaji wanaokumbwa na changamoto ya upatikanaji wa malisho, jambo linalochangia migogoro baina ya makundi hayo.

“Tukiwa viongozi ambao pia ni wakulima na wafugaji, tunathamini sana mchango wa SUA, tumeshuhudia namna SUA inavyotoa elimu ya vitendo kuhusu uzalishaji wa malisho bora na namna ya kuyaendeleza, hii ni elimu muhimu sana kwa wafugaji wa sasa,” amesema Mhe. Ndemanga.

Amebainisha kuwa matumizi ya mbegu bora za malisho zinazotokana na tafiti za SUA yanaweza kuwasaidia wafugaji kuachana na mfumo wa kuhamahama wakitafuta malisho, na badala yake kutumia maeneo madogo kuzalisha chakula cha kutosha kwa mifugo yao.

“Kwa mfano, ekari moja ya ardhi inaweza kugawanywa katika sehemu nne, kila sehemu inatumika kwa zamu kulishia mifugo, na baada ya matumizi, sehemu hiyo inamwagiliwa ili irejee katika hali yake ya kawaida, hii husaidia kuhakikisha chakula cha mifugo kinapatikana mwaka mzima,” amesema Mkuu wa Wilaya.

Kwa upande wake SUA, imeendelea kutumia tafiti na utaalamu wake kutoa suluhisho la kisayansi kwa changamoto ya malisho kwa mifugo, ikiwa ni sehemu ya juhudi zake za kusaidia kuboresha maisha ya wakulima na wafugaji nchini, na kupunguza migogoro ya mara kwa mara kati ya makundi hayo.



 

Post a Comment

0 Comments