SUAMEDIA

Wahitimu SUA wajivunia ujuzi walioupata, wajipanga kwa kujiajiri kabla ya mahafali

 

Na: Josephine Mallango

Wahitimu wa Shahada ya Familia na Afya ya Mlaji pamoja na Shahada ya Maendeleo ya Jamii kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wamesherehekea kwa shangwe kumaliza mitihani yao ya mwisho, wakifurahia mafanikio yao kwa burudani mbalimbali chuoni hapo huku wakitoa shukrani kwa walimu waliowaongoza katika safari yao ya kitaaluma.

Wakizungumza baada ya kumaliza mitihani yao, baadhi ya wahitimu wameeleza namna wanavyojipanga kujiajiri wakisubiri Maafali yanayotarajiwa kufanyika mwezi Novemba mwaka huu.

Irene Paul Emanuel, mhitimu wa Shahada ya Familia na Afya ya Mlaji, amesema amejiandaa kuingia moja kwa moja kwenye ujasiriamali kwa kutumia kipaji chake cha upambaji (makeup).

"Siwezi kurudi nyumbani nikae, nataka nikifika nyumbani nanunua vifaa vya makeup na kuanza kazi, walimu wetu wametufundisha kuwa wabunifu na kujitegemea, nitajitangaza kupitia mitandao ya kijamii na kuwafuata wateja wangu kokote walipo kwa sababu nimefundishwa kitaalamu, nitatoa huduma ya kiwango cha juu tofauti na watu wanaopaka makeup kwa mazoea. Najua nitafanikiwa kabla ya maafali,” amesema Irene.

Kwa upande mwingine, Happiness Shababi Sillo, ambaye pia ni mhitimu wa Shahada ya Familia na Afya ya Mlaji, amesema ujuzi alioupata chuoni umemfungulia milango mingi ya kujiajiri.

"Nimejifunza kushona viatu, mabegi, nguo za aina mbalimbali, pamoja na kutengeneza mapambo ya ndani ya nyumba, shule na kwenye shughuli za chakula (catering), nina uwezo wa kutengeneza mapambo ya kipekee na kupanga mazingira ya kuvutia, huu ujuzi unaweza kunifanya niajiriwe au nijiajiri mwenyewe," amesema kwa matumaini makubwa.






Post a Comment

0 Comments