SUAMEDIA

Naibu Katibu Mkuu wa Elimu Zanzibar aipongeza SUA, aomba Kampasi Zanzibar

 

Na: Josephine Mallango

Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali Zanzibar, Khalid Masoud Wazir, amesema kuwa fursa zinazopatikana katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ni muhimu sana na zinapaswa kutangazwa zaidi, kwani zina mchango mkubwa katika kukuza uchumi wa nchi.


Amesema hayo wakati wa majumuisho ya ziada ya siku chuoni SUA, ambapo ametembelea baadhi ya vitengo muhimu vya Chuo hicho vikiwemo Kituo cha Utafiti na Mafunzo ya Uchumi wa Buluu, Kitengo cha Mifugo, Kitengo cha Bustani, Jengo Mtambuka la Mafunzo la Dkt. Samia, Kitengo cha Teknolojia ya Kufundishia, SUGECO, pamoja na Kituo Atamizi cha Vijana.

Naibu Katibu Mkuu huyo amesema SUA ina  majibu ya mikakati ya utekelezaji wa Serikali zote mbili kwa kuwa inawaongezea wataalam ujuzi na kutoa ajira kwa vijana za kujiajiri wenyewe kutokana na mitaala yao na ufundishaji uliojaa vitendo unaosababisha vijana wanaoamaliza kuwa na uwezo wa kujiajiri.


 “Hiki Chuo namna nilivyofika na nilivyotembea imenipa mtazamo tofauti na awali ni Chuo kikubwa mno na kina majibu ya utekelezaji wa mikakati ya Serikali hasa kule Zanzibar kuna suala la uchumi wa bluu umefanyika uwekezaji mkubwa na  umekamilika ila imebaki suala la ujuzi bado tuna wataalam wachache lakini kwa namna nilivyoona hapa SUA ufugaji wa samaki , kilimo ikiwemo cha matikiti maji  na mboga mboga, haya mambo  yazidishiwe kutangazwa ili yafike kila mahala yataendelea kusaidia utatuzi wa uchumi wa nchi ”, amesema Mhe. Wazir.

Kutokana na umuhimu wa elimu ya vitendo kwa maendeleo ya uchumi wa buluu na sekta ya kilimo, Naibu Katibu Mkuu huyo ameuomba uongozi wa SUA kuanzisha kampasi ya SUA Zanzibar ili kusaidia vijana wengi zaidi kupata ujuzi unaohitajika kwa wakati huu.


Kwa upande wake, Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha SUA, Prof. Raphael Chibunda, alisema kuwa kwa sasa SUA ina ushirikiano wa karibu na Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA), na kwamba idadi ya wanafunzi kutoka Zanzibar wanaojiunga na SUA inaongezeka mwaka hadi mwaka.

Prof. Cibunda amesema SUA kinaendelea kuwa Chuo cha mafunzo kwa vitendo  na  wahitimu kutoka SUA wana uwezo wa kujiajiri wenyewe  ama kuajiriwa na kuweza kuingia katika ushindani wa soko  la ajira popote kutokana na wanavyoandaliwa chuoni hapo . 



Post a Comment

0 Comments