SUAMEDIA

SUA yazindua Mitaala mipya sita kukuza Ualimu wa Masomo ya Amali, wanafunzi wahimizwa kujiunga

 Na: Farida Mkongwe

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimetangaza rasmi mitaala mipya sita inayolenga kuwaandaa walimu wa kufundisha masomo ya amali katika shule za msingi na sekondari, kufuatia mabadiliko makubwa ya sera ya elimu na mitaala nchini.

Makamu Mkuu wa SUA, Prof. Raphael Chibunda akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani)

Akizungumza na waandishi wa habari Julai 22, 2025 chuoni hapo, Makamu Mkuu wa SUA, Prof. Raphael Chibunda, ameeleza kuwa mitaala hiyo mipya imeundwa kwa weledi mkubwa ili kuhakikisha Taifa linapata walimu stadi watakaoendana na mabadiliko ya mfumo wa elimu unaolenga kutoa maarifa na ujuzi kwa vitendo.

“Leo tumewaita mahususi kuwaeleza watanzania kuhusu kuanzishwa kwa mitaala mipya sita inayojibu mahitaji ya mabadiliko ya elimu nchini, hii ni hatua kubwa katika kuhakikisha tunaandaa walimu mahiri wa kufundisha masomo ya amali kwenye shule zetu,” amesema Prof. Chibunda.

Prof. Chibunda amesema mitaala hiyo mipya imeshaidhinishwa na Tume ya Vyuo Vikuu Tanzania (TCU) na kwamba SUA inakuwa Chuo cha kwanza kutekeleza maagizo ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia ya kuandaa mitaala na kufundisha walimu wa masomo ya amali baada ya kubainika kwa  changamoto kubwa ya uhaba wa walimu wenye sifa na ujuzi wa kufundisha masomo hayo.


Ameitaja mitaala hiyo kuwa ni Shahada ya Ufundishaji wa Uzalishaji wa Mazao ya Kilimo (Bachelor of Crop Production with Education),  Shahada ya Ufundishaji wa Ushonaji na Mitindo ya Mavazi (Bachelor of Textiles and Clothing with Education na Shahada ya Ufundishaji wa Bustani na Mboga (Bachelor of Horticulture with Education).

Mitaala mingine ni pamoja na Shahada ya Ufundishaji wa Lishe na Huduma ya Chakula (Bachelor of Nutrition and Catering with Education), Shahada ya Ufundishaji wa Ufugaji wa Viumbe wa Majini, (Bachelor of Aquaculture with Education) na Shahada ya Ufundishaji wa Uzalishaji wa Mifugo (Bachelor of Livestock Production with Education)

Kwa upande wake Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa Taaluma, Utafiti na Ushauri wa kitaalamu, Prof. Maulidi Mwatawala amesema kuzinduliwa kwa programu mpya za Shahada zinazochanganya ualimu na stadi za amali ni hatua kubwa ya kimkakati itakayokuza na kuchochea ajira na ujasiriamali nchini.

 Naibu Makamu Mkuu wa Chuo upande wa Taaluma, Utafiti na Ushauri wa kitaalamu, Prof. Maulidi Mwatawala  akizungumza katika mkutano huo

“…..mitaala yetu kama tulivyosema sehemu kubwa ni mafunzo kwa vitendo wanajifunza ualimu lakini anajifunza kwa vitendo zile stadi zenyewe za kilimo kwa hiyo ukiacha kuajiriwa hata yeye mwenyewe ana uwezo wa kujiajiri kwa sababu atakuwa na stadi za kutosha ambazo anaweza kutumia kuanzisha miradi mbalimbali iwe ya kilimo iwe ya mifugo….”, amesema Prof. Mwatawala

Naye Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Masomo ya Shahada za Awali kutoka SUA Dkt. Hamis Juma Tindwa, amewahimiza waombaji  wa nafasi za masomo kuwasilisha maombi yao kwa njia rahisi na ya kidijitali kupitia tovuti rasmi ya Chuo hich0 ambayo ni www.sua.ac.tz, ambapo watakutana na maelekezo ya namna ya kuomba huku akiwataka wasisite kuwasiliana na Chuo kwa msaada, akisisitiza kuwa SUA iko tayari kuwaongoza kufanikisha ndoto zao za kitaaluma.

Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Masomo ya Shahada za Awali kutoka SUA Dkt. Hamis Juma Tindwa akifafanua kuhusu Mitaala mipya


Post a Comment

0 Comments