SUAMEDIA

SUA yawataka waombaji wa kozi ya BLS kukamilisha maombi Mapema

 

Na: Hadija Zahoro

Kuelekea muhula mpya wa masomo 2025/2026, Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kupitia Idara ya Maikrobaolojia, Parasitolojia na Bioteknolojia kimewataka waombaji wa kozi ya Shahada ya Sayansi ya Bioteknolojia na Sayansi za Maabara (BLS) kuhakikisha wanakamilisha mchakato wa maombi mapema, kutokana na ongezeko kubwa la wanafunzi wanaotaka kujiunga na programu hiyo.

Akizungumza mubashara kupitia kipindi maalum cha udahili kwa wanafunzi kinachorushwa na  SUA FM, Mkuu wa Idara hiyo, Dkt. Augustino Alfred Chengula amesema kuwa kozi hiyo hutolewa SUA pekee nchini na ina nafasi kubwa ya kumuwezesha mhitimu kujiajiri au kuajiriwa.

Dkt. Chengula amesema Chuo kina uwezo wa kudahili takribani wanafunzi 100 wa moja kwa moja kutoka ngazi ya kidato cha sita na wanafunzi 40 kutoka ngazi ya stashahada, lakini kutokana na ongezeko la waombaji na mahitaji ya kitaaluma, SUA imekuwa ikiongeza udahili hadi kufikia wanafunzi 200 kwa mwaka.

Ameeleza kuwa kozi ya Sayansi ya Bioteknolojia na Sayansi za Maabara inajikita katika matumizi ya teknolojia ya kisasa kwenye viumbe hai, hasa vimelea, kwa lengo la kuboresha maisha ya kila siku ya binadamu na wanyama.

Aidha, wahitimu wa programu hii huandaliwa kitaaluma na kwa vitendo kufanya kazi katika maeneo mbalimbali ya maabara, zikiwemo hospitali, kliniki za wanyama, taasisi za utafiti, na pia kujiajiri kwa kufungua maabara binafsi.

‘‘Tunatoa elimu ambayo imejikita zaidi kumuwezesha mhitimu aweze kufanya kazi kwa vitendo pale anapomaliza ndiyo maana tunasema kwamba si lazima aende VETA kwani ujuzi anaopata hapa unajitosheleza kabisa kumuwezesha kwenda kufanya kazi moja kwa moja bila kupata changamoto yoyote’’ amesema Dkt. Chengula.

Programu ya Shahada ya Sayansi ya Bioteknolojia na Sayansi za Maabara (BLS) ilianza kutolewa rasmi SUA mwaka 2004, ikichukua muda wa miaka mitatu hadi kuhitimu ambapo tangu kuanzishwa kwake, imekuwa kivutio kwa waombaji wengi nchini kutokana na umahiri wa wahitimu wake ambao wameendelea kufanya vizuri katika sekta mbalimbali.

Post a Comment

0 Comments