Na: Siwema Malibiche
Menejimenti ya Chuo Kikuu cha
Sokoine cha Kilimo (SUA), ikiongozwa na Makamu Mkuu wa Chuo, Prof. Raphael
Chibunda, imetembelea na kukagua mwenendo wa utekelezaji wa Mradi wa Elimu ya
Juu kwa Mageuzi ya Kiuchumi (HEET), ambao unaendelea vizuri kuelekea kukamilika
kwake.
![]() |
Makamu Mkuu wa Chuo Prof. Raphael Chibunda (kulia) akipewa maelezo ya maendeleo ya utekelezaji wa Mradi wa HEET (Picha zote na Ayoub Mwigune) |
Akizungumza na SUA Media Julai 22,
2025 wakati wa ziara hiyo katika Kampasi za Solomon Mahlangu na Edward Moringe
mkoani Morogoro, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Mipango, Utawala na
Fedha, Prof. Amandus Muhairwa, amesema kuwa ameridhishwa na maendeleo ya kazi
inayofanyika na amesisitiza kuwa wakandarasi wanapaswa kuongeza kasi ya
utekelezaji huku wakizingatia weledi na viwango vya ubora vinavyotakiwa.
Prof. Muhairwa amebainisha kuwa
hadi sasa utekelezaji wa mradi huo umefikia kati ya asilimia 20 hadi 40, na
kuongeza kuwa moja ya faida kuu zinazotarajiwa kutokana na mradi huo ni
kuongezeka kwa miundombinu ya kisasa kama vile madarasa ambayo yataboresha
mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi.
![]() |
Makamu Mkuu wa Chuo Prof. Raphaeli Chibunda (kulia) akiwa na Naibu Makamu Mkuu wa Chuo anayeshughulikia Mipango, Utawala na Fedha, Prof. Amandus Muhairwa (kushoto) katika ukaguzi wa Mradi |
Kwa upande wake, Naibu Mratibu wa
Mradi wa HEET-SUA, Dkt. Winfred Mbungu, amesema kuwa utekelezaji wa mradi huo
unafanyika katika kampasi zote tatu za SUA.
Ameeleza kuwa kama sehemu ya timu
ya usimamizi, imeendelea kufuatilia kwa karibu maendeleo ya kila hatua kwa
kufanya ukaguzi wa mara kwa mara na kushughulikia changamoto zinazojitokeza
huku wakizingatia utunzaji wa mazingira.
Mradi wa HEET ambao unatekelezwa
kwa muda wa miaka mitano (2021–2026), unakadiriwa kugharimu zaidi ya shilingi
bilioni 73. Baada ya kukamilika kwake, SUA inatarajia ongezeko kubwa la udahili
wa wanafunzi, kuwafikia watu wenye mahitaji maalum na jamii kwa ujumla katika
kampasi zake zote.
0 Comments