SUAMEDIA

Wafugaji chukueni tahadhari ya ugonjwa wa Homa ya Kiwele - Dkt. Temba

 Na: Ayoub Solomon Mwigune

Wafugaji wa Halmashauri ya Mji Njombe wametakiwa kuchukua tahadhari mapema dhidi ya ugonjwa wa Homa ya Kiwele ‘Mastitis’ unaoathiri Ng’ombe wa maziwa. 

Akizungumza na wafugaji wa Halmashauri hiyo, Dkt. Benigni Temba, Mhadhiri na mtafiti wa Mradi wa NANOCOMM, amesema Homa ya Kiwele ina aina mbili ambazo ni ile inayoonekana kwa dalili kama uvimbe, joto na maumivu, na ile isiyo na dalili za wazi lakini hupunguza ubora wa maziwa.

“Homa ya Kiwele isiyo na dalili ni hatari zaidi kwa sababu haionekani kwa macho, hivyo vipimo vya maabara ni muhimu kwa utambuzi sahihi. matibabu yanapaswa kufanyika mapema na dozi za dawa kukamilishwa,” amesema Dkt. Temba.

Naye Afisa Mifugo wa Halmashauri ya Mji Njombe, Bi. Frida Mlowe, amewashukuru wataalamu wa SUA kwa kutoa mafunzo na kufanya uchunguzi wa ugonjwa huo katika halmashauri hiyo. Amesema elimu iliyotolewa itasaidia wafugaji kudhibiti homa ya kiwele kwa ufanisi.

Wafugaji waliopata mafunzo, Fedrick Gaspa na Ally Kitogela, wamesema kuwa elimu waliyoipata imesaidia kuelewa changamoto za ugonjwa huo na  hatua za kuchukua ili kuboresha uzalishaji wa maziwa na kuongeza kipato.

Mradi wa NANOCOMM unatekelezwa katika mikoa ya Tanga, Iringa, Mbeya, Njombe na Arusha. Tafiti zinazofanywa zinawalenga wafugaji kubaini vyanzo vya homa ya kiwele na kutafuta tiba mbadala za kuudhibiti ugonjwa huo nchini.







Post a Comment

0 Comments