SUAMEDIA

SUA yapanda miti takribani Ishirini elfu (20,000) kuboresha vyanzo vya maji

 Na: Siwema Malibiche

Wananchi Mkoani Morogoro wametakiwa kuilinda misitu ya hifadhi kwa kuepuka kufanya uharibifu kutokanao na shughuli za kibinadamu  ikiwemo ukataji ovyo wa miti kwa ajili ya maandalizi ya mashamba ili kutunza uoto wa asili.

Mkuu wa  Wilaya ya Morogoro Bw. Mussa Kilakala akipanda mti katika Msitu wa Hifadhi wa Kimboza (Picha zote na Nickolous Roman)

Wito huo umetolewa na Mkuu wa  Wilaya ya Morogoro Bw. Mussa Kilakala wakati akizindua    Mradi wa Urejeshwaji wa Mazingira Asilia Hifadhi za Misitu ya  Kimboza na Ruvu ambapo  zoezi la  upandaji wa miti  katika  huo litasaidia kuboresha vyanzo vya maji.

Kwa upande wake, Mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Sokoine Cha Kilimo SUA, Dkt. Charles Kilawe, ambae pia ni Mkuu wa  Mradi  amesema kuwa jukumu lao kama mradi ni kuoteasha miti sehemu ilizoharibiwa kwa lengo kuendelea kutunza uoto wa asili.

 Mkuu wa  Mradi Dkt. Charles Kilawe (kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Morogoro Bw. Kilakala (katikati) wakitete jambo

Dr. Kilawe ameongeza kuwa miti mingi ya asili hupotea katika misitu nchini  kwa sababu ya uwepo wa mimea vamizi mfano Misedelea ambayo kitaalamu hushauriwa kupandwa mbali na hifadhi ya misitu    huku akitambua umuhimu wa misitu kwa jamii husika ikiwemo upatikanaji wa  dawa za asili.

Kwa upande wao,  Wanafunzi wa Shahada ya Awali ya  Sayansi ya Misitu kutoka SUA Bw. Charles Malendeja na Bi, Miriam Mwashoma wamewataka wanafunzi kuwa na tabia ya kupanda miti   katika mazingira ya nyumbani na misitu  huku wakitambua kuwa misitu inafaida kubwa kwa jamii.

Naye, Mhifadhi Mwandamizi wa  Misitu Wilaya ya Morogoro Bw. Stanley Kweka amempongeza Dkt. Charles Kilawe kutoka SUA kwa kuja na mradi utakaoisaidia jamii kurejesha miti ya asili ambayo inapotea  huku akitambua kuwa  uwepo wa ushirikishwaji thabiti  wa jamii katika utunzaji wa misitu Mkoani Morogoro

Katika uzinduzi huo wanafunzi kutoka wa Shahada ya Awali ya Sayansi ya Misitu  zaidi ya 180 kutoka SUA wameshiriki katika upandaji wa miti  takriban 20,000 kwa kushirikiana na wanakijiji na wadau mbalimbali wa Mazingira na misitu kwa ujumla.

Mradi huo unadhaminiwa na Programu ya Ruzuku Ndogo za Mfuko wa Mazingira Duniani (The Global Environment Facility Small Grants Programme (GEF SGP) na unatekelezwa kwa pamoja na Shirika la Uhifadhi Mazingira kwa Jamii na Wanyamapori (ECOWICE), Chuo Kikuu Cha Sokoine cha Kilimo (SUA) na Wakala wa Misitu Tanzania (TFS) na unasimamiwa na Dr. Charles Kilawe.

Picha chini ni matukio mbalimbali katika upandaji wa miti










Post a Comment

0 Comments