Na: Siwema Malibiche
Rais Mstaafu wa
Jamhuri ya Afrika Kusini Mhe. Thabo Mbeki amefanya ziara maalumu katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha
Kilimo (SUA) kwa kutembelea Kampasi ya
Solomon Mahlangu kama alama ya uhusiano kati ya Tanzania na Afrika Kusini ambao uliasisiwa na waasisi ya Uhuru wa nchi hizo.
![]() |
Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Afrika Kusini Mhe. Thabo Mbeki akipanda mti katika eneo la makaburi ya wapigania uhuru wapinania uhuru wa Afrika Kusini |
Ugeni huo kutoka Afrika ya Kusini umepokelewa na
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ambaye pia ni Waziri Mkuu Mkuu Mstaafu Mhe. Jaji
Joseph Sinde Warioba na viongozi wengine wa Chuo akiwemo Makamu Mkuu wa Chuo
Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda Mei 22,2025 Mkoani Morogoro
ambapo wameeleza kuwa menejmenti ya Chuo itaendelea kuhifadhi miundombinu ambayo
imeachwa na wapigania Uhuru wa Afrika ya Kusini
kwa faida ya vizazi vijavyo.
Akizungumzia mara baada kufika SUA Rais huyo
Mstaafu wa Jamhuri ya Afrika Kusini Mhe. Thabo Mbeki ameupongeza uongozi wa SUA na Mkoa wa Morogoro kwa kuendelea kutunza historia ya wapigania uhuru wa Africa ya Kusini na historia yake huku akitamani historia hiyo iendelee kurithishwa kwa vizazi
vijavyo kwa maslahi ya nchi zote mbili.
![]() |
Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ambaye pia ni Waziri Mkuu Mkuu Mstaafu Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba akiweka mashada kwenye makaburi ya wapigania uhuru wa Afrika Kusini |
Rais huyo
Mstaafu wa Jamhuri ya Afrika Kusini aliambatana na viongozi mbalimbali wa kiserikali, wanafunzi kutoka katika Chuo Kikuu cha Africa
Kusini na waandishi wa habari ambapo amesisitiza kuwa nchi
hiyo inatambua kilichowahi kufanywa na mkoa wa Morogoro na Tanzania kwa ujumla kipindi cha
kupigania uhuru wake.
Kwa upande wake, Naibu Makamu Mkuu wa Chuo Taaluma, Utafiti na Ushauri wa Kitaalamu Prof. Maulid Mwatawala amemshukuru Rais huyo Mstaafu wa Jamhuri ya Afrika Kusini Mhe. Thabo Mbeki kutembelea katika hospitali iliyokuwa ikitumika kutoa huduma za kiafya kwa wapigania Uhuru wa Africa Kusini na kuongeza kuwa kama menejmenti ya Chuo itaendelea kutunza na kuhifadhi hospitali hiyo.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo Prof. Raphael Chibunda akisalimiana na Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Afrika Kusini Mhe. Thabo Mbeki wa Afrika Kusini |
Aidha, Rais Mstaafu wa Jamhuri ya Afrika Kusini
Mhe. Thabo Mbeki ameweka mashada ya maua katika makaburi na kupanda mti kando ya makaburi ya wapigania uhuru wa Taifa hilo ikiwa ni ishara ya kuthamini
jitihada walizozifanya kwa nchi hiyo na kutunza mazingira.
Katika Kampasi ya Solomon Mahlangu ugeni huo kutoka Afrika ya Kusini umetembelea maeneo mbalimbali waliyokuwa wanayatumia kipindi cha kupigania uhuru ikiwemo hospitali na makaburi ya wapigania Uhuru wa Chama cha ANC ambapo wameonesha heshima kwa kupanda mti na kuweka mashada.
0 Comments