SUAMEDIA

Waandaji wa vitabu vya elimu kwa Wakulima watakiwa kuzingatia mpango wa uandaaji wake.

 Na: Calvin Gwabara – Morogoro.

 Imeelezwa kuwa Mipango sahihi na uandaaji wa vifaa vya mafunzo ina mchango mkubwa katika kuhakikisha ujifunzaji mzuri na uhaulishaji wa maarifa kwa wakulima.

Prof. Athman Kyaruzi Ahmad kutoka Idara ya Ugani wa Kilimo katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) akizungumza na Wanafunzi hao

Hayo yamebainishwa na Prof. Athman Kyaruzi Ahmad kutoka Idara ya Ugani wa Kilimo katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) wakati wa mafunzo ya mradi wa AGRISPARK, kwa Wanafunzi wanaopewa mafunzo ya kuandaa vijitabu vidogo vinavyolenga kutoa majibu ya changamoto mbalimbali na mbinu bora za kilimo  kwa wakulima nchini.

Akizungumza na wanafunzi watafiti hao wa mradi, Prof. Kyaruzi alisisitiza kuwa malengo yaliyoainishwa vyema husaidia katika kupanga maudhui yanayohitajika, yenye manufaa, na rahisi kueleweka kwa wakulima ili waweze kuyatumia kuboresha shughuli zao za kilimo.

“Ni muhimu kutambua walengwa wa vitabu hivyo kabla ya kuandaa nyenzo za mafunzo iwe ni wakulima wadogo, maafisa ugani, au wanafunzi wa kilimo ili kuhakikisha kuwa maudhui yanawiana na mahitaji yao, kiwango chao cha elimu, na maarifa waliyonayo," alifafanua Prof. Kyaruzi.

Kwa mujibu wa Prof. Ahmad, uchaguzi wa aina sahihi ya vifaa vya mafunzo ni muhimu kwa ujifunzaji wenye tija kwa kwakuwashauri Wanafunzi hao kufikiria kwa kina kuhusu muundo unaofaa kwa wakulima, ikiwa ni vijitabu vyenye picha, mwongozo wa hatua kwa hatua, au nyenzo za rejea na kusisitiza kuwa lugha iwe nyepesi na inayoeleweka na iwe na mifano halisi ili wakulima waweze kuelewa na kutumia maarifa hayo kuboresha kilimo chao.

Akizungumzia umuhimu wa kuweka malengo bayana ya mafunzo katika maandalizi ya vifaa vya elimu amesem kuwa malengo haya yanapaswa kuwa yanayopimika na yanayoweza kufikiwa, yakilenga kuongeza ujuzi wa wakulima, kuboresha mbinu zao, na kuhimiza mabadiliko chanya katika kilimo.

Kuhusu mpangilio na uwasilishaji wa maudhui, Prof. Ahmad aliwataka Wanafunzi watafiti kuhakikisha kuwa taarifa zinafuata mtiririko mzuri, huku dhana ngumu zikivunjwa katika sehemu rahisi kueleweka na kuwataka kutumia michoro, vielelezo, na mifano halisi ili kusaidia wakulima, hasa wale wenye ujuzi mdogo wa kusoma na kuandika, kuelewa vyema.

Pia mbobevu huyo kwenye masuala ya Kilimo na Ugani kutoka SUA alisisitiza umuhimu wa kufanyia majaribio vifaa hivyo kabla ya kusambazwa kwa wingi.

"Kabla ya kusambaza vijitabu hivi kwa kiwango kikubwa, ni muhimu kuvijaribu kwa kundi dogo la wakulima ili kutathmini ufanisi wake kwani maoni yao yatasaidia kuboresha maudhui ili yawe ya vitendo na yanayokidhi mahitaji yao," alisema Prof. Kyaruzi.

Mradi wa AGRISPARK, unaosimamiwa na SUA, unalenga kuziba pengo la maarifa ya kilimo kwa kuwawezesha wanafunzi watafiti kuandaa nyenzo za elimu kwa wakulima na  kupitia mpango huu, wakulima wadogo kote Tanzania wanatarajiwa kupata taarifa zilizopangiliwa vizuri na zenye msingi wa tafiti ili kuongeza uzalishaji na kukabiliana na changamoto kuu za kilimo

 PICHA WASHIRIKI WAKIFUATILIA MAFUNZO HAYO







Post a Comment

0 Comments