SUAMEDIA

AGRISPARK yawajengea uwezo Wanafunzi namna ya kutambua mahitaji ya wakulima

 Na: Calvin Edward Gwabara – Morogoro.

Wanafunzi wa mafunzo katika mradi wa AGRISPARK wametakiwa kuhakikisha kuwa vitabu vinavyoandaliwa kwa ajili ya wakulima lazima viwe vinaeleweka kirahisi, Elimu yake inatekelezeka, na vinapatikana kwa urahisi kupitia utambuzi mzuri wa walengwa wa vitabu hivyo kwa kuzingatia  kutumia lugha rahisi, mifano inayofaa, na vielelezo ili kuongeza uelewa na matumizi ya maarifa ya kilimo kwa wakulima.

Mtafiti mwenza wa mradi wa AGRISPARK, Dkt. Nicholous Mwalukasa akifundisha namna ya kutambua mahitaji ya wakulima kabla ya kuwaandalia vitabu vya elimu.


Kauli hiyo imetolewa na mtafiti mwenza wa mradi wa AGRISPARK, Dkt. Nicholous Mwalukasa, alipokuwa akiwaelekeza wanafunzi wa mradi juu ya uchambuzi wa hadhira na jinsi ya kujihusisha na jamii za wakulima kabla ya kuanza kuandaa vitabu vya elimu kwa wakulima.

Dkt. Mwalukasa aliendesha mafunzo hayo kwa njia shirikishi, akiwawezesha wanafunzi kupata ujuzi muhimu wa kuwafikia na kuwasiliana kwa ufanisi na wakulima na kusisitiza umuhimu wa kuelewa mahitaji ya wakulima, changamoto zao, na upendeleo wao wa kupata taarifa ili kuboresha usambazaji wa maarifa ya kilimo na kuwapa taarifa halisi wanazozihitaji.

Wanafunzi walifundishwa mbinu mbalimbali za uchambuzi wa hadhira, ikiwa ni pamoja na tafiti za maoni, mahojiano, na majadiliano ya vikundi lengwa na kuwaeleza kuwa ili taarifa za kilimo ziwe na matokeo chanya, lazima zilingane na mahitaji mahususi ya wakulima kwa kuzingatia mambo kama vile eneo, mbinu za kilimo, viwango vya elimu, na upatikanaji wa teknolojia za mawasiliano.

“Kutengeneza maudhui ya elimu ya kilimo kwa wakulima pekee hakutoshi, bali ni muhimu sana kutambua wakulima wenyewe vizurina mahitaji yao ili huhakikisha kwamba taarifa hizo ndizo wanazozihitaji na zitaweza kutumiwa kuboresha kilimo chao,” alisisitiza.

Mbali na maarifa ya kutambua wakulima, Wanafunzi walifanya na mazoezi ya vitendo ili kuboresha ujuzi wao ambapo walipewa madodoso ambayo wakulima wamejaza kwenye utafiti wa awali wa mradi huo ili kuweza kuzitumia kuchambua na kutambua ili kujua hali halisi za wakulima wanaotarajia kuwaandalia vitabu hivyo kabla ya kwenda kukutana nao watakapomaliza mafunzo lengo likiwa kuwasaidia wanafunzi kupata ujasiri na umahiri wa kukusanya taarifa muhimu moja kwa moja kutoka kwa wakulima.

"Wakulima mbalimbali wana viwango tofauti vya upataji wa taarifa, kuanzia vyombo vya habari vya asili kama redio na maafisa ugani, hadi majukwaa ya kidijitali kama vile simu za mkononi na mitandao ya kijamii hivyo lazima mfikirie njia nyingi za kusambaza maarifa ya kilimo ili kuhakikisha kuwa taarifa zinawafikia wakulima kwa njia rahisi na inayoeleweka," alieleza.

Baada ya mafunzo, Wanafunzi walieleza kufurahishwa kwao na mafunzo hayo na walikiri kuwa uchambuzi au kutambua wahusika na vitabu hivyo yaani wakulima na  ushirikishwaji mzuri ni sehemu muhimu za ugani wa kilimo na mawasiliano.


PICHA ZA WASHIRIKI WAKIFUATILIA MAFUNZO HAYO






Post a Comment

0 Comments