SUAMEDIA

SUA yaendelea kuimarisha mafunzo kwa vitendo ili kuzalisha wataalamu wabobezi

 Na: Siwema Malibiche

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeendelea kuhakikisha mafunzo kwa vitendo  yanafanyika kwa ubora  na ufanisi  mkubwa ili kuzalisha wataalamu wabobezi watakaoisaidia jamii kwa kutoa huduma bora itakayopelekea maendeleo kwa Taifa.



Hayo yamesemwa na Mhadhiri  kutoka Ndaki ya Tiba ya Wanyama na Sayansi ya Afya  iliyopo SUA Dkt.  Mungo Ngalameno  alipozungumza na SUA Media  wakati wa  mitihani ya vitendo inayoendelea kufanyika katika  Kampasi ya Edward Moringe mkoani Morogoro ikihusisha  wanafunzi wa mwaka wa kwanza kutoka Shahada ya Awali ya Utabibu wa Wanyama ambapo amesema SUA inatengeneza misingi bora kwa kuzalisha wataalamu wenye ufanisi na ubora kwa jamii.

Aidha Dkt. Ngalameno ameupongeza uongozi wa Chuo hicho kwa kuendelea kuboresha miundombinu  ya kujifunzia kwa wanafunzi ikiwemo maabara na vifaa vyake  na kusema Wahadhiri wanaendelea kuhakikisha wanafunzi kutoka chuoni hapo wanakuwa na ubora utakaosaidia kutibu wanyama  na kuisaidia jamii inayowazunguka huku akijivunia kuwepo kwa  wataalamu wengi wa tiba ya wanyama nchini katika Sekta mbalimbali waliozalishwa SUA.


Kwa upande wake Mwanafunzi wa Shahada ya Awali ya Utabibu wa Wanyama Bakiri Azizi amekiri kufurahishwa na kuwepo kwa mafunzo kwa vitendo kwani anaamini yatamsaidia kutatua changamoto kwa urahisi na kuwataka wale wote wanaotamani kujiunga na masomo yao SUA waweze kujiunga ili wafaidike na elimu bora inayotolewa na Chuo hicho.



Naye Mwanafunzi wa Shahada ya Awali ya Utabibu wa Wanyama  SUA Gradness Roman amesema anajivunia kuwa SUA na anatamani  idadi ya wanafunzi wanawake iongezeke kwani bado kumekuwa na imani potofu kuwa wanawake hawawezi kusoma masomo ya udaktari wa wanyama.

Mafunzo kwa vitendo SUA hufanyika kwa ufanisi kutokana na kuwepo kwa miundombinu na uangalizi mkubwa wa walimu kulingana na masomo husika ili kuzalisha wataalamu wenye ujuzi, weledi na ubora unaotakiwa kwa maendeleo ya taifa.







Post a Comment

0 Comments