SUAMEDIA

SUA kuendelea kumuenzi Hayati Sokoine kwa kutoa tafiti zenye tija

 

Na: Farida Mkongwe

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeahidi kuendelea kumuenzi Hayati Edward Moringe Sokoine ambaye alikuwa Waziri Mkuu wa Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuendelea kutoa elimu bora na kufanya tafiti zinazosaidia kuleta ufanisi na tija kwa Taifa na kutatua changamoto zinazowakabili wananchi hususan watanzania waishio vijijini.

Rais wa Jamhuri ya Mungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akizindua kitabu cha Edward Moringe Sokoine Maisha na Uongozi Wake , kushoto ni mtoto wa Hayati Sokoine na Balozi wa Tanzania nchini Canada Joseph Sokoine

Ahadi hiyo imetolewa Septemba 30, 2024 na Makamu Mkuu wa Chuo hicho Prof. Raphael Chibunda wakati akitoa maelezo mafupi kuhusu Mradi wa Tawasifu za Viongozi wakati wa uzinduzi wa Kitabu cha Hayati Edward Moringe Sokoine kiitwacho “Edward Moringe Sokoine: Maisha na Uongozi Wake”  katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa cha Julius Nyerere jijini Dar Es Salaam.

“SUA tunajivunia mafanikio makubwa katika kutoa mchango wa kuinua maisha ya watanzania,  aidha tunaamini kuwa kupitia kitabu hiki ambacho Chuo chetu kimepewa nafasi ya kushiriki katika uandishi wake, vizazi vijavyo vitapata mwanga kuhusu dhamira ya Sokoine ya kuleta mabadiliko chanya katika jamii”, amesema Prof. Chibunda.


Akizungumzia uzinduzi wa kitabu hicho wakati akitoa salamu za familia ya Hayati Sokoine, Balozi wa Tanzania nchini Canada Joseph Sokoine amemshukuru Rais Samia pamoja na wote walioshiriki kufanikisha kitabu hicho kikiwemo Chuo Kikuu cha SUA na kusema kuwa hatimaye ndoto ya karibu miaka 40 ya kusoma kitabu cha Hayati Sokoine imetimia na kwamba kizazi cha sasa na kijacho kinaweza kupata historia ya kiongozi huyo.

Hayati Edward Moringe Sokoine alikuwa ni Waziri Mkuu wa Tatu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, aliwahi kuwa Waziri Mkuu mara mbili, tangu tarehe 13 Feb hadi 7 Nov, 1980 na mara ya pili kuanzia tarehe 24 Feb, 1983 hadi 12 April 1984 alipofariki dunia kutokana na ajali ya gari.













Picha ya kwanza ya Mhe. Rais ni kwa hisani ya Ikulu, picha zingine na mpiga picha wetu Gerald Lwomile

Post a Comment

0 Comments