SUAMEDIA

Wazazi na walezi wametakiwa kuwapeleka vijana wao wenye changamoto ya lugha SUA kujifunza

 

 Na: Farida Mkongwe

Wazazi na walezi wenye vijana ambao wanataka kujiunga na vyuo vikuu lakini wanaona vijana wao wana changamoto katika masuala ya matumizi ya lugha wametakiwa kufika katika Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) ili kutatua changamoto hizo kupitia Idara ya Taaluma za Lugha iliyopo Ndaki ya Sayansi za Jamii na Insia chuoni hapo.

                            

Kauli hiyo imetolewa na Mhadhiri Mwandamizi kutoka Idara hiyo Dkt. Job Mwakapina wakati akizungumza na SUA Media kwenye Maonesho ya Nanenane Kanda ya Mashariki yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Nyerere mjini Morogoro.

Dkt. Mwakapina amesema katika Idara yao kuna Kituo cha Lugha za Kiafrika na za Kimataifa ambacho kinatoa huduma mbalimbali zikiwemo kozi za muda mfupi za miezi mitatu au minne za lugha ya kiingereza na kiswahili na pia wanashirikiana na vyuo vingine duniani kutoa mafunzo ya muda mfupi kwa lugha za kijerumani, kiarabu na kifaransa.

                          

”Pia Kituo hiki kinafanya tafiti katika lugha hizi ambazo nimezisema hivyo nitoe wito tu kwa wazazi na walezi hasa katika kipindi hiki ambapo vijana wanasubiri kwenda chuoni kama kijana hayupo vizuri kwenye lugha basi mlete sisi tutamuandaa vizuri ataenda chuoni akiwa safi”, amesema Dkt. Mwakapina.

Huduma nyingine zinazotolewa na kituo hicho ni kutafsiri maandiko, kutoa mafunzo ya maandalizi kwa ajili ya mitihani ya kimataifa ya kiingereza, kutoa huduma ya ukarimani kutoka Kiswahili kwenda kiingereza au kutoka kiingereza kwenda kifaransa.

“Hicho ni kituo kimoja lakini kituo cha pili ni cha mambo ya kijinsia ambacho kinatoa huduma ya kujenga uelewa kwa jamii inayotuzunguka juu ya mambo ya kijinsia, kufanya tafiti mbalimba katika maeneo ya jinsia na kutoa mafunzo ya muda mfupi yanayohusiana na jinsia”, amesema Dkt. Mwakapina.

 

 











Post a Comment

0 Comments