SUAMEDIA

SUA yaiomba Serikali kuwezesha watafiti ili wafanye tafiti nyingi zenye manufaa kwa taifa.

 


Na: Farida Mkongwe

Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (SUA) kimeiomba Serikali ifikirie namna ya kuwawezesha wataalam wa utafiti nchini kwa kuwapa ufadhili ili waweze kufanya tafiti nyingi zenye maslahi na manufaa kwa taifa.    

                                                                                                                                                                                                      

Ombi hilo limetolewa na Mkuu wa Chuo hicho Waziri Mkuu Mstaafu na Makamu wa Kwanza wa Rais Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba wakati akitoa salaam za Chuo kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa uzinduzi wa Jengo Mtambuala la Mafunzo Agosti 6, 2024 katika Kampasi ya Edward Moringe Sokoine mjini Morogoro.

                                                                                                                                                                                            

Mhe. Jaji Warioba amesema watafiti pamoja na kufanya kazi nzuri katika tafiti zao wanakabiliwa na changamoto ya kupata ufadhili wa ndani hali inayowapa ugumu kufanya tafiti zao katika maeneo mbalimbali nchini kwa kuwa wafadhili kutoka nje wana masharti na maeneo yao wanayotaka yafanyiwe utafiti.

                                

  “Sehemu kubwa ya utafiti inafadhiliwa na watu wa nje, asilimia 92 ya fedha zinazotumika kwenye utafiti zinatoka kwa wafadhili wa nje, fedha zetu ni  asilimia 8 tu, lakini wafadhili kutoka nje wana maeneo yao hivyo sisi tukitaka kufanya utafiti kwa maeneo ya humu ndani kwa maana ya Tanzania hatuna uwezo”, amesema Mhe. Jaji Warioba

                                

Aidha Mhe. Warioba amezungumzia umuhimu wa tafiti zinazofanywa na watafiti mbalimbali kufika kwa walengwa ili matunda ya matokeo ya tafiti hizo yaweze kuinufaisha jamii na taifa kwa ujumla.

“Matokeo ya utafiti wakati mwingine yanabaki hapa hapa nadhani ifike wakati tuanze kuweka utaratibu ambao matokeo ya utafiti unaotokea hapa yaweze kufika katika vitengo vinavyohusika ambapo itasaidia katika kuandaa Sera na kufanya mipango ya maendeleo”, amesema Mhe. Jaji Warioba.

                              

                                   

  







Post a Comment

0 Comments